1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kwa nini matamasha ya Bobi Wine huzuiliwa?

Lubega Emmanuel20 Desemba 2018

Waziri wa masuala ya ndani Uganda, asema Bobi Wine huzuiliwa kuendesha matamasha yake kwa sababu yeye hukiuka masharti ya usalama anayowekewa.

https://p.dw.com/p/3ARbe
Uganda Parlament Debatte über Alter für Präsidialamt
Picha: DW/L. Emmanuel

Waziri wa masuala ya ndani Uganda alasiri ya leo amefafanua bungeni kuwa msanii na mbunge Bobi Wine huzuiliwa kuendesha matamasha yake kwa sababu yeye hukiuka masharti ya usalama anayowekewa.

Waziri alikuwa akiwasilisha majibu ya ni kwa nini msanii na mbunge Bobi Wine huzuiliwa kufanya matamasha ilihali inafahamika hicho ndicho chanzo cha kipato chake tangu zamani.

Hii ni kufuatia malalamiko aliyowasilisha bungeni msanii huyo mwanasiasa akidai kuwa sababu za yeye kutendewa hivi ni hila za kisiasa. 

Tangu alivyojitosa katika siasa, msanii Robert Kyagulanyi almaarufu Bobi Wine amekuwa akipata shida kufanya matamasha yake ya muziki. Chanzo cha haya yote ni mienendo ya vyombo vya usalama hususan polisi kuzuia matamasha hayo na kumtia katika hasara kubwa kutokana na gharama anazotumia kuziandaa.Kufuatia mfululizo wa visa vya kuzuia matamasha yake Bobi Wine aliwasilisha malalamiko bungeni.

Waziri wa Usalama Uganda, Jenerali Elly Tumwine akizungumza na waandishi wa habari
Waziri wa Usalama Uganda, Jenerali Elly Tumwine akizungumza na waandishi wa habariPicha: DW/E. Lubega

Spika wa bunge Rebbecca Kadaga naye alielezea kushangaa kwake kuhusu tabia ya polisi kumtatiza Bobi Wine na mashabiki wake kujumuika.

Jambo ambalo liliwaudhi wabunge ni jawabu alilotoa waziri wa usalama Jenerali Elly Tumwine kwamba mienendo ya polisi na vyombo vingine kuzuia matamasha ya msanii huyo kiongozi wa vuguvugu la "People Power" ni mojawapo ya hatari za kikazi anazokumbana nazo mtu yeyote yule. Wabunge wengi waliona kuwa jibu hilo ni kejeli.

Alasiri ya leo waziri wa usalama aliyeagizwa na waziri mkuu kutoa sababu za Bobi Wine kutatizwa katika kuendesha matamasha yake akifafanua kuwa ni kutokana na mbunge huyo kukiuka masharti ya usalama wa raia na mali zao amesema.

Wakati huohuo, shirikisho la wasanii Uganda limewasilisha malalamiko kuhusu vitendo hivyo kwa spika wa bunge wakiitaka serikali kulegeza masharti hayo hasa msimu wa tafrija.Lubega Emmanuel DW Kampala

Mhariri: Saumu Yusuf