1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kura yaandaliwa kwa amani kanda ya Kusini mwa Tanzania

28 Oktoba 2020

Zoezi la upigaji kura limefanyika kwa hali ya amani na utulivu katika mikoa ya Kanda ya Kusini mwa Tanzania licha ya kuwepo kwa taarifa za vitisho kutoka kwa baadhi ya watu wanaodaiwa kutaka kufanya vurugu

https://p.dw.com/p/3kYS5
Tansania | Präsidentschaftswahlen
Picha: Ericky Boniphace/DW

Akitoa tathmini ya hali ya usalama katika zoezi la upigaji kura kwa waandishi wa habari saa kadhaa zilizopita, kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Mtwara ACP. Mack Njera amesema  zoezi la upigaji kura limefanyika vizuri kwenye maeneo mbali mbali. Kuhusu hali ya matishio Mack Njera amesema hakuna tukio lolote kubwa ambalo limeripotiwa linalohusu uvunjifu wa amani kwa wananchi na ulinzi wa kutosha umeimarishwa katika maeneo yote, huku akiwahakikishia usalama wananchi wakati wote.

Tansania Singida | Wahlen | Tundu Antiphas Lissu
Tundu Lissu- Mgombea urais wa CHADEMA akipiga kuraPicha: Said Khamis/DW

Hata hivyo licha ya tume ya taifa ya uchaguzi nchini Tanzania (NEC) kuandaa mazingira na vifaa vya wapiga kura kwa watu wenye uhitaji maluumu, baadhi ya walemavu kutoka kundi la watu wasioona wamedai kukabiliwa na changamoto ya kutopiga kura kwa siri kutokana na kutopewa karatasi za nukta nundu ambazo ziliandaliwa kwa ajili ya kundi hilo.

DW, ilipita kujionea hali ya mwamko wa upigaji kura katika baadhi ya maeneo Mkoani Mtwara na kukuta vituo vingi wakati wa mchana vikiwa havina watu huku baadhi ya vijana wakilaumiana kutojitokeza katika vituo vya kupigia kura. Ijapokuwa muda wa zoezi la kupiga kura umekamilika baadhi ya wananchi ambao walikuwepo kwenye vituo vya kupigia kura kabla ya wakati huo waliendelea na upigaji kura.