1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kundi la wanamgambo la CODECO lasababisha mauaji ya 17 Bunia

27 Machi 2023

Kundi sugu la wanamgambo la CODECO Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, limewauwa watu 17 waliowateka nyara katika eneo hilo linalokumbwa na vita vya kati ya wanajeshi wa serikali na waasi wa M23.

https://p.dw.com/p/4PJqb
Milizsoldaten bewaffnete Gruppe URDPC/CODECO
Picha: Alexis Huguet/AFP/Getty Images

Watu hao walioawa walitekwa nyara katika eneo la Djugu kilomita 45 Kaskazini mwa mji wa Bunia jimboni Ituri, hii ikiwa ni kulingana na kiongozi wa Bunia, Banguneni Gbalande, aliyezungumza na shirika la habari la AFP.

Gbalande ameongeza kwamba taarifa zaidi za waliouwawa alizipata moja kwa moja kutoka kwa familia ya waathiriwa. Kiongozi mwengine, Toko Kagbanese alithibitisha mauaji ya watu hao 17.

Kulingana na mkaazi mmoja wa Bambu, moja ya vijiji viwili vilivyoshambuliwa siku ya Jumamosi, watu hao walitekwa nyara baada ya wanachama watatu wa CODECO kuuwawa baada ya kushambuliana na kundi jingine la waasi. Miongoni mwa waliotekwa nyara ni mwamamke mja mzito.

Watu 5 wauawa katika shambulizi la majambazi mashariki mwa DRC

CODECO ni kundi sugu la wanamgambo katika Jamhuri ya kidemokrasia ya Congo linalofanya operesheni zake katika eneo lililo tajiri kwa madini nchini humo.  Tangu mwishoni mwa mwaka 2022 makumi ya watu wamekuwa wakiuwawa kila wiki katika eneo la Ituri.

Katika wiki za hivi karibuni wapiganaji wa kundi hilo la wanamgambo wamekuwa wakilaumiwa, kwa misururu ya mauaji yakiwemo ya wanawake na watoto. Kundi hilo linadai kuwalinda jamii ya walendu kutoka kwa kundi jingine la kikabila la Hema pamoja na jeshi la DR Congo.

Wanamgambo mashariki mwa DRC wauwa watu wapatao 15

Eneo la Mashariki mwa Congo limekuwa ngome ya makundi tofauti ya waasi wengi, wakianzisha vita vilivyogeuka kuwa vita vya kikanda na kuyumbisha mahusiano ya kidiplomasia kati ya Congo na baadhi ya jirani zake tangu miaka ya 1990 na 2000.

Ituri ni jimbo ambalo mapigano hayo yamekuwa yakiripotiwa mara kwa mara na kusababisha mauaji ya watu wengi.

Chanzo: afp