1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Polisi ya Uganda ipo kidete kwa kitisho cha ugaidi.

5 Septemba 2023

Vyombo vya usalama nchini Uganda vinaendelea na operesheni ya kutafuta mabomu ya kutengenezwa kienyeji nyumbani ambayo inadaiwa yalipangwa kutumiwa na magaidi kuendesha mashambulizi katika maeneo mbalimbali ya nchi.

https://p.dw.com/p/4VyUQ
Uganda Kampala Bombenanschlag auf Kirche verhindert
Picha: ABUBAKER LUBOWA/REUTERS

Wakati huohuo, raia wamechukua tahadhari zaidi na ni kutokana na mwitikio huo ndipo mabomu mengine sita yamegunduliwa na baadhi kuteguliwa kwa usalama wa hali ya juu. Jumapili iliyopita katika jiji la Kampala kulipatikana bimu kwenye kanisa moja na mshukiwa mmoja kukamatwa akidaiwa alikuwa anapanga kuilipua ndani ya kanisa hilo lililokuwa na watu zaidi ya elfu moja.

Baada ya kupata taarifa zaidi kwamba wenzake wanne walikuwa wanajiandaa kulipua sehemu zingine za mji, askari wa vyombo vya usalama wameimarisha operesheni na kufanikiwa kupata mabomu mengine sita pamoja na kuwakamata washukiwa kwenye mitaa mbalimbali ya mji.

Hali ya tahadhari kwa kila raia.

Uganda Kampala Bombenanschlag auf Kirche verhindert
Mtaalamu wa kutegua mabomu akiwa kazini nchini UgandaPicha: ABUBAKER LUBOWA/REUTERS

Kwa upande wao, raia wamechukua tahadhari kuhakikisha kuwa wako chonjo na macho wakishuku mikoba yoyote wanayogundua sehemu mbalimbali ikiwemo majengo ya maduka, sehemu za kuabudu na zinginezo zilizo na mikusanyiko mikubwa ya watu.

Wamiliki wa sehemu za starehe nao wamechukua tahadhari hasa katika kipindi hiki ambapo ligi maarrufu za bara Ulaya zinawavutia mashabiki kujumuika sehemu hizo. Haya ni baadhi ya maoni ya watu.

ADF na madai ya kufanya ugaidi Uganda.

Kwa mujibu wa taarifa za polisi, kundi la waasi la ADF ndilo linadaiwa kuhusika katika njama hizo za kuendesha mashambulizi ya kigaidi. Hii ni baada ya harakati za kutokomeza kundi hilo Mashariki mwa Uganda kushika kasi hivi karibuni.

Wiki kadhaa kabla ya matukio haya ya majaribio ya mashambulizi ambayo wananchi wanataka kuamini kuwa yametibuliwa, mataifa ya magharibi yalitoa tahadhari wa raia wao walioko Uganda kuchukua tahadhari.

Soma zaidi:Uganda yatibua shambulizi la bomu kanisani

Yalitaja kuwa palikuwa na taarifa za kijasusi kuwa vitendo vya ugaidi vingefanyika nchini Uganda. Vyombo vya usalama vinaelezea kuwa tahadhari hiyo ilikuwa muhimu na walianzisha juhudi za kukabiliana nalo na ndiyo maana wamefaulu hadi sasa kudhibiti hali.

Chanzo: DW Kampala