1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaSudan

Sudan yamuita nyumbani balozi wake wa Kenya

5 Januari 2024

Sudan imemuita nyumbani balozi wake nchini Kenya ikipinga hatua ya Rais William Ruto ya kufanya mazungumzo na kamanda wa wanamgambo wa RSF Mohamed Hamdan Daglo.

https://p.dw.com/p/4asEC
Kiongozi wa RSF aendelea kuzuru mataifa ya Afrika kusaka uungwaji mkono
Jenerali Mohamed Hamdan Daglo akiwa atika moja ya mikutano yake na waandishi wa habari katika makao makuu ya RSF, mjini KhartoumPicha: MOHAMED NURELDIN ABDALLAH/REUTERS

Kwenye taarifa iliyorushwa na shirika rasmi la habari la SUNA, kaimu Waziri wa Mambo ya Nje wa Sudan Ali al-Sadiq amesema balozi huyo amerejeshwa nyumbani kwa mashauriano ya kupinga mapokezi rasmi yaliyoandaliwa na serikali ya Kenya kwa ajili ya kiongozi huyo wa wanamgambo.

Amesema mashauriano hayo yataangazia uwezekano wa namna hatua hiyo inavyoweza kuathiri uhusiano kati ya Kenya na Sudan.

Dagalo, ambaye vikosi vyake vinapambana na jeshi la Sudan linaloongozwa na Abdel Fattah al-Burhan amekua ziarani katika baadhi ya mataifa ya Afrika ambayo ni pamoja na  Uganda, Ethiopia na Djibouti, Kenya na sasa yuko Afrika Kusini.

Sudan bado haijapata suluhu ya mzozo unaowakabili licha ya juhudi za kimataifa
Jenerali Abdul Fattah al-Burhan (kushoto) na Mohamed Hamdan Dagalo(kulia) ambao wanazozana nchini Sudan hali iliyobua mzozo mbaya wa kibinaadamu. Picha: Bandar Algaloud/Mahmoud Hjaj/AA/picture alliance

Uhusiano baina ya Burhan na serikali ya Kenya umekuwa katika mvutano kwa miezi kadhaa, wakati Nairobi ikiangazia kuendeleza mawasiliano na Daglo ili kusuluhisha mzozo baina ya majeshi hayo mawili ya Sudan.

Soma pia: Vikosi vya RSF nchini Sudan vimefanikiwa kuingia Wad Madani

Katika hotuba yake ya Januari 1, Jenerali Burhan alionya kwamba serikali za Afrika zinazoandaa ziara za "wauaji hao" "zinajionyesha dhahir kuwa ni washirika katika mauaji ya watu wa Sudan".

Juhudi za upatanishi kwa kiasi kikubwa zimesimama katikati ya ongezeko la uadui kati ya majenerali hao wawili.

Vita hivyo vimesabaisha vifo vya zaidi ya watu 12,000, hii ikiwa ni kulingana na makisio ya taasisi ya Armed Conlfict Location and Dat Event Project, huku zaidi ya watu milioni 7 wakilazimika kuyakimbia makazi yao, umesema Umoja wa Mataifa.