1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kiongozi wa Hezbollah amshambulia mfalme wa Saudi Arabia

4 Januari 2022

Kiongozi wa kundi la wanamgambo la Hezbollah nchini Lebanon, Sayyid Hassan Nasrallah, amemshambulia kwa maneno mfalme wa Saudi Arabia akisema Riyadh ilisaidia kueneza itikadi kali ya Kiislamu duniani.

https://p.dw.com/p/457EK
Libanon Hisbollah Scheich Hassan Nasrallah Ansprache in Beirut
Picha: dapd

Na inawashikilia mateka maelfu ya Walebanon wanaofanya kazi katika eneo hilo  lenye utajiri wa mafuta la Ghuba ya Uajemi. 

"Mfalme gaidi, uliyesafirisha itikadi ya Kiwahabi ya kundi la Daeshi duniani, na ni wewe gaidi uliyetuma maelfu ya Wasaudi kufanya mashambulizi ya kujitoa muhanga Iraq na Syria, na ni wewe ndiye uliyeanzisha vita vya miaka saba dhidi ya watu masikini wa Yemen, na kuwaua watoto, wanawake na kuharibu watu na majengo. Ni wewe gaidi unayesimama na Marekani katika vita vyake vyote na kufungua ardhi zao na vituo vyao vya kijeshi kufanya vita vyake dhidi ya wanadamu."

Nasrallah amesema haya wakati wa hotuba yake mjini Beirut kujibu maoni ya Mfalme Salman, ambaye aliwataka Walebanon kukomesha kile alichokiita "udhibiti wa magaidi wa Hezbollah'' nchini Lebanon katika hotuba yake ya wiki iliyopita.

soma Mzozo wa Iran na Saudi Arabia wakolezwa baada ya vita vya Yemen

Juhudi za kurekebisha mahusiano

Karte Saudi Arabien Abqaiq EN

Maoni haya yanajiri katika wakati ambapo mamlaka za Lebanon zinajaribu kurekebisha mahusiano na Saudi Arabia ambayo yaliharibika mwezi Oktoba wakati nchi hiyo ilipomtaka balozi wake mjini Beirut kurejea nyumbani na kupiga marufuku uingizaji wote wa bidhaa kutoka Lebanon.

Hatua hiyo ya Saudia ilikuwa ni kujibu shutuma zilizotolewa na Waziri wa Habari wa Lebanon, George Kordahi, katika mahojiano ya televisheni moja nchini humo akisema kwamba vita vya Yemen vilikuwa ubatili na uchokozi wa muungano unaoongozwa na Saudi Arabia.

Mapema mwezi uliopita, Kordahi ambaye alitoa maoni hayo kabla hajachukua kazi hiyo, alijiuzulu wadhifa wake lakini hatua hiyo haikuponya majeraha katika mvutano huo.

Mzozo wa Yemen ulianza mwaka 2014 baada ya waasi wa Kihouthi kuchukua udhibiti wa mji mkuu, Sanaa, ambapo pia wanadhibiti sehemu kubwa ya kaskazini mwa nchi.

Muungano unaoongozwa na Saudi Arabia uliingia vitani mwaka uliofuata ukitaka kuirejesha madarakani serikali inayotambulika kimataifa na kuwaondoa waasi.

Kauli ya Nasrallah haiwakilishi serikali

Libanon | Regierungsbildung | Premierminister Najib Mikati
Waziri Mkuu wa Lebanon Najib MikatiPicha: Bilal Jawich/Xinhua/picture alliance

Waziri Mkuu wa Lebanon Najib Mikati alitoa taarifa akisema maoni ya Nasrallah hayawakilishi serikali wala walio wengi wa nchini Lebanon na kutoa wito kwa wanasiasa wa Lebanon kuachana kutoa kauli ambazo hazina msingi.

Na sasa kumekuwa na wasiwasi nchini Lebanon kwamba mvutano huo unaweza kuathiri maelfu ya Walebanon wanaofanya kazi katika taifa hilo la Ghuba.

soma Mamia warejea nyumbani katika ubadilishaji wafungwa Yemen

Balozi wa Saudia nchini Lebanon, Waleed Bukhari, alijibu mara moja baada ya hotuba ya Nasrallah kupitia Twitter, akisema maoni ya kiongozi huyo wa Hezbollah ni ya "uongo ambao hauwezi kufichwa gizani.''

Hata hivyo, Bukhari hakumtaja Nasrallah moja kwa moja, bali alimtaja kama Abu Raghal, jina la mtu ambaye kwenye historia ya Waarabu anatambuliwa kama alama ya uhaini.

 

Vyanzo/AP, Reuters