1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kenya na Tanzania kushirikiana katika vita dhidi ya Covid-19

Shisia Wasilwa5 Agosti 2021

Kenya na Tanzania zitashirikiana kukabiliana na ugonjwa wa COVID-19 ambao virusi vyake vinazidi kubadilika kila uchao huku visa vya maambukizi vikizidi kuongezeka.

https://p.dw.com/p/3ybIg
Tansanina | COVID-19 Impfstoff aus der COVAX Initiative
Picha: Domasa Sylivester/AP/picture alliance

Kenya na Tanzania zitashirikiana kukabiliana na ugonjwa wa COVID-19 ambao virusi vyake vinazidi kubadilika kila uchao huku visa vya maambukizi vikizidi kuongezeka. Kwenye taarifa ya pamoja ya mawaziri wa Afya wa Kenya Mutahi Kagwe na mwenzake wa Tanzania Dkt. Dorothy Gwajima wamesema, huu ni mwanzo wa ushirikiano mkubwa kati ya mataifa hayo katika kukabiliana na kuenea kwa virusi vya corona. 

Masuala mengine yaliyojadiliwa na mawaziri hao ni pamoja usafirishaji wa bidhaa kupitia mipakani, vibali vya kuingia na kutoka kupitia mipakani kwa raia wa mataifa ya Kenya na Tanzania na mikakati ya kukabaliana na virusi vya Corona.

Soma zaidi: Tanzania yaanza utoaji chanjo ya Corona kitaifa

Mazungumzo hayo yamefanyika baada ya ziara ya Rais wa Tanzania Samia Suluhu mwezi wa tano mwaka huu nchini Kenya ambapo yeye na Rais Uhuru Kenyatta waliahidi kuboresha mahusiano ya mataifa hayo. Waziri wa Afya nchini Kenya Mutahi Kagwe, anafafanua.

“Huu ni mwanzo wa muendelezo wa ushirikiano wetu. Mgeni wetu atazuru baadhi ya vituo vyetu vya afya, kuangalia nyanja nyingine za afya ambazo tunaweza kushirikiana.”

Gwajima ameutetea msimamo wa aliyekuwa Rais wa Tanzania hayati John Magufuli  

Tansania Daressalam | Coronavirus | Impfung Samia Suluhu Hassan, Präsidentin
Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan akichomwa chanjo ya Covid-19Picha: Emmanuel Herman/REUTERS

Waziri wa Afya wa Tanzania Dkt. Dorothy Gwajima ambaye yuko nchini Kenya kwa ziara rasmi ya siku moja, ameutetea msimamo wa aliyekuwa Rais wa Tanzania hayati John Pombe Magufuli wa kukabiliana na virusi hivyo.

Utawala wa Hayati Magufuli, ulikuwa umepinga kutumika kwa chanjo kwa hofu ya kuwepo na nia iliyojificha pamoja na matumizi ya barakoa. Dkt Dorothy, amebainisha kuwa wangali wanachanganya mbinu za asili na za kisayansi kukabiliana na ugonjwa huo, licha ya kupigia debe matumizi ya chanjo dhidi ya Covid-19.

“Tiba asili zinaendelea kutumika, kuboresha, vita vya huyo mdudu, kwa kuongeza vitamin C, tulizokunywa. Kujifukuza, angalia hali yako, wameshatoa utaratibu pale Muhimbili, ni mtu yupi ambaye anaweza kufanya hivyo. Kwa hivyo hatubomoi, na hatukanyi tulichokifany. Tulianza nacho kama silaha ya awali na sasa tuko katika silaha nyingine. Ukienda vitani huruhusiwi kuenda na kisu na fimbo hata kama kuna ak-47. Kazi bado inaendelea.”

Utawala wa hayati Magufuli, hukuwa ukitoa idadi ya visa vya maambukizi pamoja na idadi ya watu walioaga dunia kutokana na ugonjwa wa Covid 19, kinyume na ilivyo sasa katika uwatala wa Rais Samia Suluhu ambaye alibuni kamati ya kukabiliana na ugonjwa huo.

"Chini ya sheria za kimataifa taifa ambalo linalomba linatakiwa kutoa  nyaraka za kuridhisha  kuwa mtuhumiwa ana hatia ambayo si ya kisiasa basi lazima taifa husika kama Uturuki kumfikisha mahakamani kufikia maamuzi hayo.Changamoto ambayo naona ni kwamba Uturuki si nchi inayojulikana kuziheshimu haki za binadamu."

Ugonjwa wa Covid 19 umebadilisha mwenendo wa maisha ya binadamu kote ulimwenguni.