1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kamati ya bunge Kenya yapendekeza mageuzi tume ya uchaguzi

27 Novemba 2023

Kamati iliyoundwa na Bunge la Kenya kushughulikia madai ya upande wa upinzani imechapisha ripoti yake ya mwisho inayotoa mwito wa mageuzi kwenye tume ya uchaguzi, masuala ya kodi na matumizi ya serikali.

https://p.dw.com/p/4ZTHx
Rais William Ruto wa Kenya na kiongozi wa upinzani nchini humo Raila Odinga
Serikali na upinzani nchini Kenya zimekuwa kwenye msuguano kwa miezi kadhaa sasaPicha: AFP

Shirika la Habari la Reuters ambalo limeiona nakala la ripoti hiyo limearifu kuwa mbali ya mageuzi ya tume ya uchaguzi kamati hiyo imependekeza kuundwe jopo litakalofanya tathmini ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2022 ambao upinzani haukuridhishwa na matokeo yake.

Serikali pia imeshauriwa kupitia upya sera zake za kikodi, kuzingatia uwiano katika matumizi ya fedha za umma na kutanua sekta ya hifadhi ya jamii ili kuwafikia watu wengi zaidi.

Kamati hiyo ya vyama vyote iliundwa mapema mwaka huu baada ya Kenya kukumbwa na wimbi kubwa la maandamano ya upinzani uliokuwa ukilalamikia matokeo ya uchaguzi uliopita, kupanda kwa gharama za maisha na viwango vya kodi.