1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Jumla waliokufa kwa joto hija imepindukia watu 1,000

23 Juni 2024

Cairo,Hadi kufikia sasa zaidi ya mahujaji 1,000 wamekufa kutokana na joto kali wakati wa Hija ya mwaka huu nchini Saudi Arabia. Takriban nchi 10 zimeripoti vifo vya watu 1,100 wakati wa ibada hiyo ya Hija.

https://p.dw.com/p/4hPLV
Saudi Arabia | Vifo vya joto wakati wa Hija ya Waislamu
Mwanajeshi wa jeshi la usalama la Saudia akiwazuia watu kukaribia huku mtu aliyeathiriwa na joto kali akilala chini huko Mina. karibu na mji mtakatifu wa Saudi Arabia wa Makka, Juni 16, 2024.Picha: FADEL SENNA/AFP/Getty Images

Hija ni moja ya nguzo tano za Uislamu ambazo Waislamu wote wenye uwezo lazima wakamilishe angalau mara moja maishani mwao.

Wanadiplomasia kutoka nchi za Kiarabu wameliambia shirika la Habari la AFP mapema wiki hii kwamba raia wa Misri 658 waliokufa wakati wa kuhiji, 630 walikwenda Makka lakini hawakusajiliwa. Rais Abdel Fattah El-Sisi amemwamuru Waziri wake mkuu Moustafa Madbouly kuchunguza kiini cha mkasa huo.

Waziri huyo Mkuu wa Misri ameamuru kampuni 16 za utalii zinyang'anywe leseni zao na mameneja wake wafikishwe kwa mwendesha mashtaka wa umma kujibu mashataka ya kuwapeleka mahujaji kwa njia haramu katika mji mtakatifu wa Makka.

Baraza la mawaziri linataka faini zitakazotozwa wahusika wa mkasa huo zipewe familia za mahujaji waliokufa. Taarifa ya baraza la mawaziri iimesema kwamba idadi kubwa ya vifo vya mahujaji wa Misri ambao hawakusajiliwa imetokana na baadhi ya makampuni ambayo yaliandaa programu za Hijja kwa kutumia viza ya ziara za kibinafsi, ambazo zinazuia wamiliki wake kuingia katika mji wa Makka.