1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroSudan

Jeshi la Sudan laahidi kujibu vikali shambulizi la RSF

7 Juni 2024

Jeshi la Sudan limesema litajibu vikali shambulizi la wanamgambo wa RSF katika kijiji cha Wad al-Noura siku ya Jumatano ambalo watetezi wa demokrasia wanasema liliwaua zaidi ya watu 100.

https://p.dw.com/p/4gkxg
UNGA | Abdel-Fattah Al-Burhan
Jenerali Abdel-Fattah Al-Burhan anayeongoza jeshi la Sudan akihutubia Hadhara Kuu ya 78 ya Umoja wa Mataifa mjini New York, Sept. 21, 2023. Picha: Craig Ruttle/AP/picture alliance

Shambulizi hilo lilikuwa ni kubwa zaidi katika msururu wa mashambulizi yaliyofanywa na RSF kwenye vijiji vidogo vidogo kote katika jimbo la Gezira linalosifika kwa kilimo, baada ya kuchukua udhibiti wa mji wake mkuu wa Wad Madani mwezi Disemba.

Taarifa ya Mkuu wa Jeshi Abdel Fattah al-Burhan inatolewa baada ya madai yaliyotolewa na wanaharakati wa eneo hilo kwamba jeshi halikwenda kuwasaidia licha ya kuomba msaada siku ya Jumatano.

Hata hivyo jeshi halikutaka kuzungumzia madai hayo hata lilipoombwa kufanya hivyo.

Afisa wa ngazi za juu wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan jana Alhamisi alitoa wito wa uchunguzi wa shambulizi hilo la Wad al-Noura.

"Licha ya hali mbaya katika mzozo wa Sudan, lakini picha zinazoonyeshwa kutoka kwenye eneo hilo zinaumiza sana," alisema Mratibu huyo wa Masuala ya Kiutu Clementine Nkweta-Salami kwenye taarifa yake.

Alikuwa akizungumzia picha zilizochapishwa na kamati ya watetezi wa demokrasia huko Wad Madani yaResistance Committee kwenye mitandao ya kijamii, ambayo imekuwa ikifuatilia mashambulizi, zilizoonyesha wahanga waliokuwa wamefunikwa tayari kwa maziko.

Sudan | Jeneräli Abdel Fattah Abdelrahman al-Burhan na Mohamed Hamdan Dagalo
Picha hii inawaonyesha majenerali wawili, Abdel Fattah al-Burhan na aliyekuwa naibu wake Mohamed Hamdan Dagalo ambao kwa sasa wanapigana na vita baina ya majeshi yao vimesababisha mzozo mkubwa wa kibinaadamuPicha: Mahmoud Hjaj/AA/picture alliance

Kulingana na kamati hiyo, watu 104 waliuawa na mamia wengine walijeruhiwa katika kijiji hicho cha Wad al-Noura, na sasa wanamgambo hao wa RSF wanaelekea kwenye vijiji vingine.

Soma Pia: Madaktari wasio na mipaka wasema watu 123 wafa kwa mapigano Sudan

Kundi hilo limewashutumu wanamgambo hao sio tu kwa kuwashambulia wanakijiji, bali pia kupora mali zao na kuwafanya wanawake na watoto kukimbilia kwenye mji jirani wa Managi kuomba hifadhi. "Watu wa Wad al-Noura waliomba msaada wa jeshi, lakini inasikitisha kwa sababu hawakuja," imesema kamati hiyo. "Haya ni matukio ya kihalifu yanayoakisi tabia ya wapiganaji kuwalenga kwa makusudi raia," ilisema sehemu ya taarifa yao.

Soma Pia: Mizozo iliopo kwenye mataifa ya Afrika imesahaulika?

Shirika la habari la Reuters lililoandika taarifa hii halikuweza kuwafikia wakazi ama maafisa wa tiba wa eneo hilo ili kuthibitisha taarifa hizi kutokana na kukatwa kwa mawasiliano ya simu.

Wanamgambo wa RSF walianzisha mapigano na jeshi la Sudan mwezi Aprili, 2023 kufuatia mzozo baina ya majenerali wawili wa jeshi na tangu hapo wamechukua udhibiti wa mji mkuu Khartoum na maeneo mengi ya magharibi mwa Sudan.

Na sasa wanataka kusonga mbele kuelekea katikati mwa Sudan, wakati Umoja wa mashirika ya Umoja wa Mataifa yakisema watu wa taifa hilo wanakabiliwa na kitisho kikubwa cha njaa.

Soma pia: Wasudani wamenasa kwenye ukatili, njaa na maradhi