1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Umoja wa mataifa hautaki kuingilia kati mgogoro wa Kashmir?

Zainab Aziz Mhariri: Amina Abubakar
17 Agosti 2019

Licha ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuzitaka India na Pakistan ziutatue mgogoro wa Kashmir baina yao, baraza hilo halikuitisha kikao rasmi na wala halikutoa tamko rasmi.

https://p.dw.com/p/3O3UU
USA Deutschland und Frankreich teilen sich Vorsitz im Sicherheitsrat der UN
Picha: picture-alliance/dpa/R. Hirschberger

Wachunguzi wamesema msimamo wa baraza hilo ni wa maji ya uvuguvugu. Wajumbe wa chombo hicho cha Umoja wa Mataifa hapo jana walikwepa kuitisha kikao cha dharura ili kuujadili mgogoro wa jimbo la Kashmir. Badala yake wajumbe hao walitoa mwito kwa India na Pakistan kuusuluhisha mzozo huo baina yao tu.

Kikao cha faragha cha hapo jana juu ya suala la  Kashmiri kilifanyika kutokana na maombi ya China  baada ya waziri mkuu wa India Narendra Modi kuyabatilisha mamlaka ya utawala wa ndani ya upande wa Kashmir unaosimamiwa na India wiki mbili zilizopita. Kila upande India na Pakistan unadai mamlaka kamili juu  ya jimbo la Kashmir. Jimbo hilo ni sehemu ya hatari inayogombaniwa na nchi hizo mbili hasimu zinazomiliki silaha za nyuklia. 

Waziri Mkuu wa India Narendra Modi
Waziri Mkuu wa India Narendra ModiPicha: Reuters/A. Abidi

Balozi wa China Kwenye Umoja wa Mataifa ametahadharisha juu ya hatari ya upande wowote kuchukua hatua inayoweza kuzidisha hali ya mvutano. Hata hivyo Waziri Mkuu wa India Narendra Modi ameutetea uamuzi aliochukua katika jimbo la Kashmir. Alielezea msimamo huo katika hotuba yake ya kuadhimisha siku ya uhuru.

Balozi wa India kwenye Umoja wa Mataifa Syed Akbaruddin amesisitiza kwamba mgogoro wa Kashmir si wa kimataifa na amemkosoa balozi wa China Zhang kwa kutoa matamshi yenye lengo la kuashiria kuwa jumuiya ya kimataifa inahusika na mgogoro wa Kashmir.

Waziri Mkuu wa Pakistan Imran Khan
Waziri Mkuu wa Pakistan Imran KhanPicha: Reuters/Mary F. Calvert

Mjumbe huyo wa India kwenye Umoja wa Mataifa ameongeza kusema kuwa mgogoro wa Kashmir ni  suala la ndani. Ameeleza kuwa mzozo huo utazingatiwa na mahakama za India na kwamba nchi yake haizihitaji taasisi za kimataifa kwa ajili ya ushauri.

Pakistan ilikuwa inatarajia kuungwa mkono kimataifa katika msimamao wake wa kupinga hatua iliyochukuliwa na India ya kuyafuta mamlaka ya utawala wa ndani katika jimbo la Kashmir. Pakistan ilitarajia kujadiliwa hatua hiyo ya India kwenye kikao rasmi cha Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa. Na hakuna ishara za kuonyesha iwapo mgogoro huo utajadiliwa mnamo siku za karibuni.

Hata hivyo  balozi wa Pakistan kwenye Umoja  wa Mataifa Maleeha Lodhi amekitathmini kikao cha baraza la usalama kuwa cha mafanikio kwa nchi yake. Balozi huyo ameahidi kuwa nchi yake itaendelea na juhudi hadi mpaka hapo haki itakaporejeshwa katika jimbo la Kashmir.

Chanzo:/ https://p.dw.com/p/3O3CG