1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rwanda: Kuanzia siasa hadi haki za binadamu na wakimbizi

20 Desemba 2023

Pendekezo la mwanasiasa mkuu wa Ujerumani kupeleka wakimbizi Rwanda liliiweka tena nchi hiyo ya Kiafrika katika mwangaza. Haya ndiyo unayohitaji kujua kuhusu Rais Paul Kagame, Rwanda na namna wakimbizi wanavyoishi huko.

https://p.dw.com/p/4aPt7
Rwanda| Rais Paul Kagame
Rais wa Rwanda Paul Kagame amejiimarisha madarakaniPicha: Trinidad Express Newspaper/AFP

Katika mahojiano ya hapo Desemba 17, mwanasiasa mashuhuri wa chama cha upinzani cha CDU hapa Ujerumani, Jens Spahn, alitowa pendekezo la nchi yake kutumia mfano wa Uingereza wa kuwapeleka waomba hifadhi nchini Rwanda wakati maombi yao yakishughulikiwa. Je, pendekezo hilo lina maana gani kwa siasa za Ujerumani?

Ingawa pendekezo hilo la Spahn lilipingwa hapo hapo na Waziri wa Mambo ya Kigeni wa Ujerumani, Annalena Bearbock, aliyeliita la "kitoto" akiwa ziarani nchini Rwanda, lakini ukweli kwamba limetolewa na mwanasiasa wa ngazi za juu wa chama ambacho hadi miaka michache nyuma kilikuwa ndicho kilichotawala kwa miongo kadhaa, unaoesha kuwa ni jambo ambalo linazungumzwa kwenye rubaa za kisiasa.

Soma pia: Waziri wa nje wa Ujerumani ajitenga na wazo la kuhamishia waomba hifahi Rwanda

Vile vile, pendekezo hili limeonesha jinsi Rwanda, taifa dogo la Afrika ya Mashariki, lilivyojijenga kama kimbilio la kimataifa kwa waomba hifadhi. Lakini kuna mambo ya kuyazingatia kuhusiana na serikali, uchumi, na hali ya haki za binaadamu nchini humo.

Muundo wa serikali ya Rwanda

Tuanze na serikali ya Rwanda, ambayo inaongozwa na Rais Paul Kagame na chama chake cha Rwandan Patriotic Front, RPF, kinachoitawala nchi hiyo yenye milima na tambarare zenye rutuba tangu kumalizika kwa mauaji ya kimbari ya mwaka 1994.

Kwenye makaratasi, ni nchi inayofuata demokrasia ya vyama vingi, lakini kwenye uhalisia, hakuna kitu kinachoitwa upinzani wa kisiasa, kama linavyosema shirika la misaada la Marekani, USAID.

DW Eco Africa — Umaskini Rwanda
Ingawa rwanda imepiga hatua kubwa za maendeleo ya kiuchumi, karibu asilimia 50 ya wakazi wake wanaichini chini ya msitari wa umaskini.Picha: DW

Ushindi wa Kagame kwenye chaguzi tatu mfululizo umekumbwa na tuhuma kadhaa za uvunjwaji wa taratibu, ukiwemo wizi wa kura na vitisho. Mwaka 2017, alitangazwa kushinda kwa asilimia 99 ya kura.

Mradi wa kimataifa unaohifadhi data za demokrasia duniani, Varierties of Democracy Projest, unaiweka Rwanda kwenye kipengele cha "udikteta wa kura". Imepewa alama nane tu kati ya 40 kwenye haki za kisiasa katika ripoti ya Uhuru Ulimwenguni ya mwaka huu wa 2023.

Soma pia: Bunge la Uingereza laridhia kupeleka wakimbizi Rwanda

Kuhusu suala la haki na uhuru, Rwanda imeridhia matamko kadhaa ya kimataifa na kikanda yanayohakikisha haki za binaadamu, ambazo zinaakisika pia ndani ya katiba na sheria za nchi hiyo.

Lakini wachunguzi kadhaa wamebainisha matukio yanayoashiria uvunjwaji mkubwa wa haki za binaadamu nchini Rwanda, yakiwemo mauaji ya makusudi, watu kukamatwa na kisha kupotezwa na serikali na mateso dhidi ya wapinzani.

Haya ni mambo yenye athari kwenye uhuru wa kujieleza na kujikusanya na yanautilia mbolea utamaduni wa kutokuwavumilia wapinzani, kwa mujibu wa shirika la haki za binaadamu la Human Rights Watch.

Haki nyingine na uhuru nchini Rwanda

Kwenye suala la uhuru wa vyombo vya habari, shirika la Waandishi wa Habari Wasio Mipaka linasema baada ya kukabiliwa na miongo kadhaa ya ukandamizaji, vyombo vya habari vya Rwanda vimesalia kuwa miongoni mwa vilivyo masikini kabisa barani Afrika, na vimeiweka nchi hiyo kuwa ya 131 kati ya 180 kwenye faharasa yake ya uhuru wa habari.

Rwanda Kigali| Muonekano wa mji mkuu
Mji Mkuu wa Rwanda, Kigali, unajulikana kwa kuwa msafi, salama na tulivu.Picha: Martina Fuchs/Xinhua News Agency/picture alliance

Kuhusiana na uchumi wa Rwanda, Kagame aliirithi nchi iliyosambaratishwa na mauaji ya kimbari yaliyoangamiza takribani Watutsi milioni moja ndani ya siku 100 tu na yenye uchumi ulioharibika kabisa.

Hadi sasa, uchumi wa Rwanda unategemea kilimo cha wakulima wadogo wadogo kwa kuwa tafauti na majirani zake, haina utajiri wa rasilimali.

Soma pia:Rwanda yaikosowa Ubelgiji kutomuidhinisha balozi wake 

Hata hivyo, kwa mujibu wa Benki ya Dunia, Kagame amefanikiwa kuimarisha uchumi na kuonesha kiwango fulani cha maendeleo kwenye maisha ya raia.

Pato la limepanda hadi asilimia 142 kutoka mwaka 2000 hadi 2020 na idadi ya watu wanaoishi chini ya mstari wa umasikini ilishuka hadi asilimia 52 kufikia mwaka 2016 na 2017. Baada ya kupunguza idadi vya akinamama na watoto, Rwanda yenye raia milioni 13 ni miongoni mwa watu wanaoishi muda mrefu zaidi katika mataifa ya Afrika yaliyo chini ya Jangwa la Sahara.

Chanzo: https://www.dw.com/a-67762463