1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Jaa la taka laporomoka Kampala na kuuwa watu 23

12 Agosti 2024

Idadi ya watu waliopoteza maisha yao katika janga la kuporomoka kwa jaa la takataka mjini Kampala imefikia watu 23 huku makundi ya waokoaji wakizidi kupoteza matumaini ya kupata manusura.

https://p.dw.com/p/4jNIw
Maporomoko ya ardhi Kampala
Shughuli za uokoaji zinaendelea huku matumaini ya kuwapata manusura yakiendelea kufifiaPicha: Simon Tumwine/XinHua/dpa/picture alliance

Wengi ni wakaazi wa mtaa huo wa Lusanja ambao husaka riziki zao kutoka kwenye takataka zinazoletwa hapo zikitokea sehemu mbalimbali za mji huo wenye idadi ya watu takribani milioni nne. 

Soma pia: Watu wasiopungua 18 wauawa katika maporomoko ya taka Uganda

Hao ni waokoaji wakiendelea kutoa maiti za watu walionaswa chini ya poromoko la rundiko la taka siku ya Jumamosi. Ni siku ya tatu za juhudi hizo za kujaribu kuwanusuru watu wanaoamika wangali wamenaswa katika nyumba zao zilizofunikwa ghafla na rundiko la taka nyakati za alfajiri wakati wengine wakiwa bado wamelala. Hadi sasa idadi rasmi ya watu waliofariki imefikia 23 na manusura 18 waliokimbizwa hospitalini. Lakini wakaazi wanaelezea kuwa watu wengi bado wamenaswa na kadri muda unavyoyoyoma, hii ikiwa siku ya tatu ya shughuli za kujaribu kuwanusuru, matumaini ya kuwapata wakiwa wangali hai yanazidi kupukutika. Wanasema.

Kuporomoka kwa jaa la takataka Kampala
Walioangamia huwa ni wakaazi wanaotafuta riziki zao kutoka kwenye takataka zinazoletwa hapoPicha: Simon Tumwine/XinHua/dpa/picture alliance

Halmashauri ya mji wa Kampala ilianzisha jaa hilo mwaka 1996. Tangu wakati huo, wakaazi wa mtaa huo na maeneo jirani wamekuwa wakilalamikia kuhusu madhara yake kwa afya zao na pia mifugo wao kutokana na  uvundo unaohanikiza sehemu kote. Lakini pia kutokana na shughuli za watu waliochukua fursa za kusaka riziki kwa kuokota baadhi ya takataka kama vile plastiki na mabaki mengine na kuziuza kwa wanaozichakata au kwa ajili ya matumizi mengine. Hivyo ndivyo mtaa ulivutia idadi kubwa ya wakaazi wakajenga nyumba jirani na dampo hilo. Nyumba hizo ndizo ambazo sasa zimefunikwa na rundiko hilo kubwa la taka. Msemaji wa wizara ya ofisi ya waziri mkuu inayoshughulikia majanga Charles Odongtho amesema hivi kuhusu hatua wanazochukua kwa sasa kuwakimbilia misaada ya dharura wakaazi hao. "Watu elfu mbili wameathirika kutoka na janga hili na mbali na kuanzisha mpango wa kuwafidia tunashurikiana na shirika la msalaba mwekundu kuwapa makao ya muda katika hema tulizokita eneo jirani."

Akitoa rambirambi zake kwa waliowapoteza jamaa zao, Rais Museveni amekosoa mwenendo wa kuwaacha watu kuishi katika maeneo hatari kama hayo. Ameagiza uchunguzi wa mara moja kubaini waliohusika katika kutelekeza majukumu yao na kusababisha dampo hilo kuwa hatari. Watu mbalimbali wamekubaliana na rais  wakisema kuwa hii si ajali ila ni uhalifu wa watendaji katika halmashauri ya mji  kupuuzilia usalama wa watu.

Mapema mwaka huu, meya wa mji wa Kampala alizuru eneo hilo na kukosoa mienendo ya ufisadi kuwa chanzo cha jaa hilo la taka kutoshughulikia ipasavyo ili hali kiasi kikubwa cha fedha hutolewa kuchakata taka hizo.