1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Israel yatahadharishwa dhidi ya kuanza kushambulia Rafah

13 Februari 2024

Rais wa Marekani na Mfalme wa Jordan wajadili hali ya Gaza na kutahadharisha dhidi ya kuanzishwa mashambulio katika mji wa Rafah,Kusini mwa Gaza ambako mamilioni ya Wapalestina wamekimbilia

https://p.dw.com/p/4cLKN
USA, Washington | König Abdullah II. Jordanien und Joe Biden
Picha: Andrew Harnik/AP/picture alliance

Hali ya vita bado inaendelea katika Ukanda wa Gaza, jeshi la Israel limesema limeuwa wanamgambo kadhaa wa Kipalestina katika mapambano yaliyotokea Kusini na katikati mwa Gaza katika kipindi cha saa 24 zilizopita. Kwa upande mwingine mamilioni ya Wapalestina katika Ukanda huo wa Gaza wanaendelea kuteseka.

Jeshi la Israel katika ripoti yake ya leo Jumanne limesema zaidi ya wanamgambo 30 wa kipalestina wameuwawa katika mji wa Khan Yunis, mji ulioko Kusini mwa Gaza na karibu kabisa na mpaka wa Rafah wa kuingia nchini Misri, ambako viongozi wa Israel wameshasema kwamba wanapanga kuchukua hatua ya kuanzisha mashambulizi ya kuwaangamiza kabisa wapiganaji wa Hamas waliobakia.

Gazastreifen | Rauchwolken nach Luftangriffen auf Rafah
Picha: MOHAMMED ABED/AFP/Getty Images

Hali ya Gaza ni tete

Hali bado inatisha kwa Wapalestina wanaoishi Gaza huku ripoti ya wizara ya afya ya eneo hilo ikionesha kwamba takriban Wapalestina 28,340 wengi wakiwa ni wanawake na watoto wameuwawa kufuatia mashambulizi ya mabomu ya Israel yanayofanywa kupitia angani na ardhini.

Wakaazi wa mji wa Kusini mwa Gaza wa Rafah bado wanashambuliwa kutokea angani  kwa mabomu na jeshi la Israel ambapo jana zaidi ya watu 100 waliuliwa na mamia ya wengine walijeruhiwa.        

Kwa upande mwingine ulimwengu unajaribu kutafuta mwafaka kufikia hatua ya kusitishwa vita hivyo, jana Jumatatu rais wa Marekani Joe Biden ambaye alikutana na mfalme Abdullah wa Jordan katika ikulu ya White House alisema Marekani inashinikiza mpango wa kusitishwa kwa wiki sita vita hivyo kati ya Israel na Hamas, kama hatua ya kuelekeampango wa  kudumu wa kusitisha vita hivyo.

USA | Jordaniens König Abdullah II trifft Joe Biden
Picha: Andrew Harnik/AP Photo/picture alliance

 

Mkutano wa viongozi hao umekuja katika wakati ambapo rais wa Marekani anaonekana kuongeza shinikizo la kuitaka Israel isithubutu kuanzisha operesheni ya kijeshi ya ardhini katika mji wa Kusini mwa Gaza wa Rafah bila ya kuwa na mpango maalum wa kuwalinda raia wapalestina.Soma pia: Israel inapaswa kutafakari kabla ya kuchukua hatua, Rafah

"Watu wengi, wengi  sana miongoni mwa Wapalestina 27,000 waliouwawa kwenye vita hivi wamekuwa ni raia wa kawaida wakiwemo maelfu ya Watoto''

Mfalme Abdullah wa Jordan ambaye kabla ya kuanza ziara kwenye mataifa ya Magharibi alizunguka Gaza kudondosha msaada wa kibinadamu amesisitiza kuhusu kusitishwa vita hivyo lakini pia kutaka Israel iache kuzuia juhudi za kuwashughulikia wagonjwa,na kupeleka msaada wa kibinadamu katika Ukanda wa Gaza.

"Tayari hali ni mbaya isiyoweza kuvumilika kwa zaidi ya watu milioni moja ambao wamesukumwa mpaka Rafah,tangu vita vilipoanza. Hatuwezi kusimama tu na kuacha hili liendelee. Tunahitaji usitishwaji vita wa kudumu,,hivi sasa. Vita hivi lazima vimalizike.

Israel yakosolewa

Sauti za viongozi mbali mbali zimeendelea kusikika za kuishinikiza na kuikosoa Israel kufuatia mashambulizi yake ya mabomu dhidi ya watu wa Gaza. Seneta wa Marekani Chris Van Hollen ambaye ni mwanasiasa maarufu kutoka chama cha rais Joe Biden cha Democrat,  ameikosoa Israel kwa kusababisha vifo vya watoto kutokana na njaa, Ukanda wa Gaza, akisisitiza kwamba kitendo cha kuzuia chakula kwa makusudi ni hatua ya dhahiri ya uhalifu wa kivita na wanaochochea hatua hiyo nio wahalifu wa kivita.Soma pia: Wasiwasi wa kimataifa waongezeka kufuatia operesheni ya Israel Rafah

USA | Pro-Palästinensische Demonstrationen gegen Offensive in Rafah in New York
Picha: Michael M. Santiago/Getty Images

Seneta huyo wa chama cha Democratic alitoa kauli hiyo jana mbele ya baraza hilo na kubaini kwamba mkuu wa shirika la mpango wa chakula duniani WFP, Cindy McCain amemthibitishia kwamba watu wa Gaza wanakufa kwa njaa,kwasababu shirika hilo limeshindwa kupata chakula cha kutosha kuwanusuru watu hao.

Ama kwa upande mwingine mkuu wa  shirika la  ujasusi la Israel,Mossad, David Barnea ameelekea Cairo leo kufanya mazungumzo na wenzake wa Misri na Marekani kuhusu pendekezo la kusitisha vita lililotolewa na Qatar.

Tayari Marekani imeshathibitisha kwamba mkuu wa CIA William Burns ameelekea Misri na watajiunga pia na waziri mkuu wa Qatar Mohammed bin Abdulrahman Al-Thani ambaye pia ndiye mwanadiplomasia wa ngazi za juu wa Qatar aliyesimamia mipango iliyopita ya usitishaji vita Gaza.

 

DW Kiswahili | Saumu Mwasimba
Saumu Mwasimba Mhariri na mtangazaji wa Idhaa ya Kiswahili ya DW