1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Israel yasema haitojizuia ikiwa Iran itaishambulia

3 Agosti 2024

Afisa wa ngazi ya juu wa idara ya usalama wa Israel ameonya kwamba nchi hiyo haitojizuia ikiwa Iran itaishambulia nchi hiyo.

https://p.dw.com/p/4j4JV
Benjamin Netanyahu (kushoto) akiwa na Mkuu wa Majeshi Herzi Halevi.
Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu (kushoto) akiwa na Mkuu wa Majeshi Herzi Halevi.Picha: Israeli Prime Minister's Office/Anadolu/picture alliance

Afisa huyo amesisitiza kuwa Israel haitojizuia ikiwa Iran itaanzisha mashambulizi ya kulipiza kisasi kufuatia mauaji ya kiongozi wa Hamas Ismail Haniyeh aliyezikwa jana mjini Doha, Qatar.

Tzachi Hanegbi, mshauri wa usalama wa Israel amelinganisha mvutano wa sasa na ule wa mwezi Aprili, ambapo Iran iliilenga Israel kwa mashambulizi makubwa ya droni zipatazo 330 na makombora ya masafa marefu.

Soma pia: Biden ahofia kusambaa kwa machafuko ya Mashariki ya Kati

Wakati huo Israel ilijizuia kujibu mashambulizi hayo kwa kuheshimu miito ya washirika wake ikiwemo Marekani.

Makombora ya Iran
Makombora ya IranPicha: Iranian Army Office/ZUMA Wire/IMAGO

Hanegbi amesisitiza kwamba kwa sasa hali ni tofauti na kuwa Israel ilijizuia mara moja na haitoweza kufanya hivyo mara mbili huku akisisitiza kuwa yeyote atakayeishambulia Israel atalipia gharama kubwa.

Hofu imekua ikiongezeka kuhusu hatari ya kutanuka kwa mzozo huo na kulitumbukiza eneo zima la Mashariki ya Kati katika vita vya kikanda.

Kiongozi Mkuu wa Iran Ayatollah Ali Khamenei aliapa kulipiza kisasi kufuatia mauaji ya Hanniyeh katika ardhi yake. Wiki hii Marekani iliihakikishia Israel kwamba itaisaidia kulinda usalama wake na kukabiliana na vitisho vyote kutoka kwa Iran.

(Vyanzo: Mashirika)