1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaIran

Iran yaonya kuhusu uvaaji wa lazima wa hijab

2 Januari 2023

Polisi nchini Iran imewaonya tena wanawake juu ya uvaaji wa lazima wa hijab hata wanapokuwa kwenye vyombo vya usafiri, vyombo vya habari vimeripoti Jumatatu hii wakati machafuko yakiendelea.

https://p.dw.com/p/4LeD6
Irak Erbil | Protest nach Tod von Mahsa Amini
Picha: Safin Hamed/AFP/Getty Images

Iran imekumbwa na na maandamano yaliyogubikwa na ghasia tangu kifo cha msichana Mahsa Amini Septemba 16 baada ya kukamatwa mjini Tehran kwa madai ya kukiuka sheria kali za taifa hilo la Kiislamu ya mavazi kwa wanawake. Tehran inayaita maandamano hayo "machafuko".

Shirika la habari la Fars lilimnukuu afisa wa ngazi za juu wa polisi ambaye alisema utekelezaji wa "hatua mpya" chini ya programu ya ufuatiliaji ya ikimaanisha "ufuatiliaji" kwa lugha ya Kiajemi imetangazwa kote nchini humo na jeshi la polisi.

Soma Zaidi:Kifo cha msichana Mahsa chazusha maandamano makubwa Iran

Mpango huo wa Nazer, ulipozinduliwa mwaka wa 2020, wamiliki wa magari walitumiwa ujumbe mfupi wa maandishi kuwaarifu kuhusu ukiukwaji wa kanuni za mavazi kwenye magari yao na kuonya kuchukuliwa hatua kali iwapo itagunduliwa kulikuwa na ukiukwaji huo kwenye magari yao.

Iran I Szenen aus den Protesten im Iran und Slogans der Demonstranten
Waandamanji wanawake nchini Iran waliopinga hatua kali za polisi kufuatia kifo cha Mahsa Amini.Picha: UGC

Lakini hata hivyo tangazo la wakati huu linaonyesha kana kwamba polisi wameondoa onyo la hatua za kisheria, hii ikiwa ni kulingana jumbe zilizosambaa kwenye mitandao ya kijamii.

"Kumeonekana mtu asiyevaa hijab kwnye gari yako: Ni muhimu kuheshimu tamaduni za jamii na kuhakikisha kwamba hili halirudiwi tena," inasomeka sehemu ya ujumbe unaotajwa kutumwa na polisi na kuchapishwa kwenye mitandao ya kijamii.

Polisi ya kijamii nchini Iran inayojulikana kama "Gasht-e Ershad" ina mamlaka ya kuingia kwenye maeneo ya umma kuhakikisha utekezaji wa kanuni kali za mavazi.

Kufuatia maandamano ya muda mrefu, wanawake katika mitaa ya mjini Tehran na kwenye viunga ambavyo havifuati kanuni hizo kali za mavazi, wameshuhudiwa wakitembea bila ya kuvaa hijab na bila ya kusimamishwa kokote.

Tangu mwezi Septemba, kulipoibuka maandamano hayo, magari ya idara hiyo ya maadili katika jeshi la polisi yenye rangi ya kijani na nyeupe hayaonekani sana katika mitaa ya Tehran.

Mapema mwezi Disemba, mwendesha mashitaka mkuu wa Iran Mohammad Jafar Montazeri alinukuliwa akisema kwamba kitengo hicho cha polisi ya maadili kimefungwa. Lakini wapiga kampeni wana mashaka juu ya kauli hiyo iliyotolewa ghafla tu kwenye moja ya mikutano.