1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Iran yaonya itajibu vikali iwapo Israel itaishambulia

20 Desemba 2021

Iran imesema sauti zilizosikika karibu na kinu chake cha nyuklia cha Bushehr zinatokana na mazoezi yake ya ulinzi wa anga huku ikionya kuwa itajibu vikali iwapo Israel itaamua kuishambulia.

https://p.dw.com/p/44aZR
Österreich | Atomgespräche mit dem Iran
Picha: Joe Klamar/AFP

Kulingana na gavana wa Bushehr, Mohammadtaqi Irani  zoezi hilo la ulinzi wa anga lilifanyika mapema leo alfajiri kukiwa na ushirikiano wa hali ya juu na jeshi la ulinzi.

Mwanzoni mwa mwezi huu serikali ya Iran ilisema ilifyatua kombora angani kama sehemu ya mazoezi yake ya kijeshi baada ya kituo cha kitaifa, kuripoti kuona mripuko mkubwa katika kinu cha kufua nishati ya nyuklia cha Natanz.

Ulaya yaiomba Iran kuharakisha mazungumzo ya nyuklia

Iran imekuwa ikiishutumu Israel kuhusika na mashambulizi ya mara kwa mara yanayolenga vituo vya mpango wake wa nyuklia, likiwemo shambulio lililitokea mwezi Aprili katika kinu cha Natanz na hata mauaji ya mwanasayansi wa taifa hilo alieshughulika na masuala ya nyuklia miaka kadhaa iliyopita. Hata hivyo Israel haijakataa wala kukubali madai hayo.

Israel yatishia kuchukua hatua za kijeshi

Kuendelea kwa juhudi za mataifa yalio na nguvu duniani kuufufua mpango wa nyuklia wa Iran wa mwaka 2015, kumeifanya Israel kutishia kuchukua hatua za kijeshi iwapo diplomasia itashindwa kuizuwiya Iran kutengeneza silaha za nyuklia, licha ya Jamhuri hiyo ya kiislamu kusema kuwa mipango yake  hiyo ni kwa matumizi ya amani.

Mwanzoni mwa mwezi huu serikali ya Iran ilisema ilifyatua kombora angani kama sehemu ya mazoezi yake ya kijeshi baada ya kituo cha kitaifa, kuripoti kuona mripuko mkubwa katika kinu cha kufua nishati ya nyuklia cha Natanz.
Mwanzoni mwa mwezi huu serikali ya Iran ilisema ilifyatua kombora angani kama sehemu ya mazoezi yake ya kijeshi baada ya kituo cha kitaifa, kuripoti kuona mripuko mkubwa katika kinu cha kufua nishati ya nyuklia cha Natanz.Picha: AEOI/ZUMA Wire/imago images

Israel pekee ndiyo inayoaminika kuwa na silaha za nyuklia katika kanda nzima ya Mashariki ya kati na Iran imeapa kujibu iwapo Israel itaamua kuishambulia kwa namna yoyote ile. 

IAEA kufunga Kamera mpya kwenye kituo cha nyuklia cha Iran

Mazungumzo ambayo sio ya moja kwa moja kati ya Marekani na Iran ya kujaribu kuyafufua makubaliano ya nyuklia ya mwaka 2015 yamepiga hatua chache tangu yalipoanza mwezi uliopita kwa mara ya kwanza tangu Iran ilipobadilisha utawala kutoka kwa Hassan Rouhani hadi Ebrahim Raisi mwezi Juni mwaka huu.

Mazungumzo hayo yanatarajiwa kuanza tena mwishoni mwa mwezi Desemba.

Makubaliano ya mwaka 2015 yaliiondolea  vikwazo vya kiuchumi Iran kwa nia ya kupunguza shughuli zake za urutubishaji wa madini ya urani.

Mwaka 2018 Marekani chini ya rais wa zamani Donald Trump ilijiondoa katika makubaliano hayo na kuiwekea vikwazo zaidi Iran hatua iliyofanya taifa hilo lijibu kwa kukiuka viwango vya urutubishaji wa  urani vilivyokuwa vimewekwa chini ya makubaliano ya mwaka 2015.