1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Iran yailaumu Marekani kwa kuingilia masuala yake ya ndani

22 Juni 2021

Iran Jumanne imeilaumu Marekani kwa kungilia masuala yake ya ndani baada ya wizara ya mambo ya nje ya Marekani wiki iliyopita kuukosoa uchaguzi wa rais katika Jamuhuri ya Kiislamu ya Iran na kusema haukuwa huru na haki.

https://p.dw.com/p/3vN4U
Iran | Präsidentschaftswahlen
Picha: Vahid Salemi/picture alliance/AP

Muhafidhina Ebrahim Raisi alijipaia asilimia 62 ya kura katika uchaguzi huo wa Ijumaa huku zaidi ya nusu ya wapiga kura wakikosa kushiriki katika kura hiyo baada ya wanasiasa wengi kunenguliwa katika kinyang'anyiro hicho. Siku iliyofuata, wizara ya mambo ya nje ya Marekani ilisema kuwa inasikitishwa na hali kwamba raia wengi wa Iran hawakuweza kushiriki katika mchakato wa uchaguzi huru na haki.

Msemaji wa serikali ya Iran Ali Rabiei amesema kuwa wanachukulia tamko hilo kama mfano wa muingilio wa masuala ya ndani ya iran na kuongeza kuwa wanalilaani. Aliongeza kuwa serikali ya Marekani haiko katika nafasi ya kuzungumza kuhusu mchakato wa uchaguzi nchini Iran ama taifa lingine lolote.

USA-Russland-Gipfel in Genf | Joe Biden
Joe Biden - rais wa MarekaniPicha: Kevin Lamarque/REUTERS

Iran na Marekani zimekuwa mahasimu kwa muda wa zaidi ya miaka 40. Mvutano kati yao uliongezeka baada ya aliyekuwa rais wa nchi hiyo Donald Trump kuliondoa taifa hilo katika mkataba muhimu wa nyuklia mnamo mwaka 2018 na kuiwekea Iran vikwazo zaidi. Mrithi wa Trump Joe Biden anapendelea kujiunga tena katika mkataba huo wa nyuklia na mataifa yaliosalia katika mkataba huo yanashiriki katika mazungumzo mjini Vienna nchini Ausria kujaribu kuuokoa.

Siku ya Jumatatu, Raisi anayeonekana  kuwa mshirika wa karibu wa kiongozi wa juu kabisa nchini humo Ayatollah Ali Khameni, alisema kuwa hataruhusu mazungumzo hayo kujivuta.