1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroIran

Iran yafanya mashambulizi dhidi ya wanamgambo Pakistan

17 Januari 2024

Iran imefanya mashambulizi kwenye ardhi ya Pakistan ikizilenga kile imesema kuwa ngome za kundi la wanamgambo wa Jaish al-Adl, ikiwa ni siku moja tangu ilipoyashambulia maeneo kadhaa ndani ya Syria na Iraq.

https://p.dw.com/p/4bLTZ
Makombora ya Iran
Makombora ya Iran Picha: Iranian Army Office/ZUMA Wire/IMAGO Images

Pakistan imearifu kuwa mashambulizi hayo ya Iran yamewauwa watoto wawili na kujeruhiwa watu wengine watatu na imeyalaani kwa matamshi makali ikisema ni "uingiliaji wa makusudi" wa anga ya nchi hiyo.

Mashambulizi hayo yanatishia kuzusha mvutano kati ya nchi hizo mbili ambazo zina mahusiano ya kidiplomasia lakini mara zote hutizamana kwa jicho la tahadhari.

Yanafuatia mengine yaliyofanywa na Iran huko Syria na Iraq ambayo serikali mjini Tehran imesema yalizilenga ngome za kundi la itikadi kali la IS na kituo cha ushushushu cha Israel.

Iraq imeghadhibishwa na mashambulizi hayo na imechukua uamuzi wa kumrejesha nyumbani balozi wake wa nchini Iran.