1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Iran kupiga kura ya urais siku ya Ijumaa

26 Juni 2024

Raia wa Iran watapiga kura siku ya Ijumaa kumchagua rais mpya miongoni mwa wagombea sita walioidhinishwa, akiwemo mwanamageuzi pekee ambaye anatumai kupambana na utawala wa kihafidhina katika Jamhuri hiyo ya Kiislamu.

https://p.dw.com/p/4hXCs
Uchaguzi Mkuu Iran
Uchaguzi huo unafanyika wakati Jamhuri hiyo ya Kiislamu inakabiliwa na changamoto za kiuchumiPicha: Morteza Nikoubazl/NurPhoto/picture alliance

Uchaguzi huo unafanyika wakati ambapo Jamhuri hiyo ya Kiislamu inakabiliwa na changamoto za kiuchumi kutokana na vikwazo vya kimataifa na pia mvutano wa kikanda juu ya vita vinavyoendelea katika ukanda wa Gaza.

Wagombea wakuu ni pamoja na spika wa bunge muhafidhina Mohammad Bagher Ghalibaf, aliyekuwa msuluhishi wa zamani katika mazungumzo ya nyuklia Saeed Jalili na mwanamageuzi pekee Massoud Pezeshkian.

Ayatollah Ali Khamenei ataka Wairan wajitokeze kupiga kura

Wengine ni pamoja na meya wa mji wa Tehran Alireza Zakani, kiongozi wa kidini Mostafa Pourmohammadi na makamu wa rais aliye madarakani Amirhossein Ghazizadeh-Hashemi.

Uchaguzi wa urais ulikuwa umepangwa kufanyika mwaka 2025 japo utafanyika mapema kutokana na kifo cha Rais Ebrahim Rais aliyefariki katika ajali ya helikopta mwezi uliopita.