1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Idadi ya wahanga wa ghasia za Afghanistan yaongezeka Aprili

19 Mei 2020

Umoja wa Mataifa umesema idadi ya raia waliouawa Afghanistan imeongezeka na kufikia 380 mwezi Aprili, ukieleza wasiwasi wake kuhusu kuzorota kwa sheria ya kimataifa kuhusu haki za kibinadamu nchini humo.

https://p.dw.com/p/3cTo6
Afghanistan Kabul Anschlag auf Beerdigung
Picha: Reuters/Parwiz

Takwimu hizo mpya zinajiri wiki moja tu baada ya shambulio katika hospitali ya akina mama wajawazito lililowaua watu 24, wakiwemo watoto wachanga.

Raia wameambatanisha ongezeko la waliouawa na kuongezeka kwa harakati za kundi la Taliban mnamo mwezi Aprili. Kwa mujibu wa ujumbe maalum wa Umoja wa Mataifa nchini Afghanistan, kundi la Taliban limesababisha vifo vya raia 208, huku vikosi vya serikali vikiwaua watu 172.

Hata hivyo msemaji wa Taliban, Zabihullah Mujahid kupitia taarifa yake, ameipinga ripoti hiyo ya Umoja wa Mataifa na kuitaja kama propanga tu ya serikali ya Kabul.

''Natoa wito kwa pande zinazohasimiana kuweka chini silaha zao na kuheshimu sheria ya kimataifa kuhusu haki za kibinadamu,'' amesema Deborah Lyons ambaye ni mjumbe maalum wa Umoja wa Mataifa nchini Afghanistan.

Afghanistan Anschlag auf Klinik von Ärzte ohne Grenzen in Kabul
Wanajeshi wa Afghanistan mjini KabulPicha: picture-alliance/dpa/R. Gul

Umoja wa Mataifa imemtuma mjumbe wake mjini Doha na Kabul ili kuishinikiza serikali ya Afghanistan kufanya mazungumzo ya amani na Taliban, mazungumzo ambayo yanatarajiwa kuanza hivi karibuni baada ya Rais Ashraf Ghani na mpinzani wake Abdullah Abdullah kutia saini mpango wa kugawanya madaraka.

Ghasia ziliongezeka nchini humo licha ya Taliban kusaini makubaliano na Marekani mnamo Februari 29 ambao sehemu yake unaitaka Marekani kuviondoa vikosi vyake vya usalama, lakini kwa kigezo kuwa kundi la Taliban kutasisha mapigano. Sio mara moja ambapo kundi la Taliban limekataa miito ya serikali ya Afghanistan ya kuweka chini silaha.

Ishara zote zinaonyesha kuwa vuta nikuvute kati ya Taliban na serikali ya Afghanistan haitakwisha hivi karibuni hasa baada ya shambulio la wiki iliyopita katika hospitali ya akina mama wajawazito. Vikosi vya usalama vya serikali ya Afghanistan vimetangaza kuanzisha mashambulizi kama sehemu ya kujilinda.

Chanzo: rtre