1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Germany kuwafukuza wanaotoa machapisho ya chuki

Hawa Bihoga
26 Juni 2024

Baraza la mawaziri wa Ujerumani limepitisha muswadawa sheria unaokusudiwa kurahisha mchakato wa kuwafukuza wahamiaji watakaobainika kuunga mkono masuala yanayotafsiriwa kuwa ugaidi.

https://p.dw.com/p/4hY4I
Ujerumani I Bundestag - Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz akitoa tamko la serikali
Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz akizungumza bungeni mjini Berlin wakati akitoa tamko la serikali, Juni 26, 2024Picha: Michael Kappeler/dpa/picture alliance

Kwa mujibu wa muswada huo hatua ya kuwaondowa wahamiaji nchini itachukuliwa  ikiwa tu mtu atathibitishwa kuwa ametenda kosa moja ambalo ni la kigaidi. Hata hivyo hukumu katika kosa la namna hiyo haitalazimisha kumfukuza nchini mtu.

Kukutwa na hatia kunaweza kujumuisha sio tu kuchapisha maudhui kwenye mitandao ya kijamii bali pia hata kuunga mkono maudhui mengine yatayotafsiriwa kuwa ni ya kigaidi kwenye mitandao ya kijamii kama Instagram, Facebook na hata Tik Tok.

Serikali ya shirikisho Ujerumani imefanya mabadiliko hayo kujibu kile kinachotajwa kuwa machapisho ya chuki  mitandaoni kufuatia mashambulizi ya kundi Hamas ya Oktoba 07 dhidi ya Israel pamoja na shambulio baya la kisu  lililotokea  katika maandamano ya kupinga Uislamu kwenye mji wa Mannheim ambapo afisa mmoja wa polisi aliuwawa.

Ujerumani I Bundestag - Kansela Olaf Scholz (SPD) akitoa tamko la serikali
Kansela Olaf Scholz amesema wageni wanaokutwa na hatia ya kushabikia ugaidi watafukuzwa mara moja kutoka UjerumaniPicha: Michael Kappeler/dpa/picture alliance

Soma pia: Kansela Merkel atoa tamko la serikali

Kufuatia mkasa huo uliotokea mapema mwezi huu, Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz alitangaza mipango thabiti ya kuhakikisha sheria zinatekelezwa.Waziri wa Mambo ya Ndani Nancy Faeser, ambaye aliwasilisha mabadiliko hayo alisema kwamba serikali inachukua hatua kali dhidi ya wenye kueneza itikadi kali na chuki dhidi ya Wayahudi  mitandaoni.

Wakosoaji wasema ni mbinu ya kuminya uhuru wa kujieleza

Hata hivyo muswada huo umekutana na vizingiti vikali nje na ndani ya Bunge la Ujerumani kutoka kwa wakosoaji wakisema, muswada huo unalenga kuminya uhuru wa kujieleza na kufananisha hatua ya kupitisha muswada huo ni kama mbinu zinazotumiwa na tawala za kimabavu.

Wataalamu wa masuala ya sheria nchini Ujerumani wametilia shaka pia muswada huo, Thomas Oberhäuser mwenyekiti wa taasisi ya wanasheria Ujerumani DAV alisema muswada huo unahitaji maelezo mengi ya kisheria ili kufafanua iwapo uchapishaji, kupendezwa kama sehemu ya kuunga mkono matamshi ya chuki kwenye mitandao ni sehemu ya ugaidi.

Ujerumani I Bundestag - Kansela Olaf Scholz akitoa tamko la serikali
Bunge la Ujerumani Bundestag likiendela na vikao vyake mjini BerlinPicha: Michael Kappeler/dpa/picture alliance

Aliongeza kwamba hiyo inaweza kuwa ni vigumu kwa watu wa kawaida kutambua kuwa machapisho fulani kwenye mitandao yanahusiana moja kwa moja na masuala ya ugaidi.

Soma pia: Tamko la serikali ya Ujerumani juu ya Afghanistan.

Kwa upande mwingine Umoja wa Askari polisi nchini Ujerumani kupitia mwenyekiti wake Jochen Kopelke ameukaribisha uamuzi huo wa Baraza la Mawaziri ambao aliuelezea kuwa ni salamu za wazi kwa wale wote wanaojihusisha na masuala ya ugaidi pamoja na wafuasi wao.

Hata hivyo aliongeza kuwa lazima polisi pamoja na mamlaka zingine zijiandae kikamilifu ili kufikia malengo ya kutekelezwa kwa sheria hiyo.

Chuki ya mtandaoni inapozidi na kuingia ulimwengu wa kweli