1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaAsia

Gavana wa Benki Kuu ya Lebanon kujiuzulu

31 Julai 2023

Gavana wa Benki Kuu ya Lebanon, Riad Salameh, ametangaza kujiuzulu, uamuzi utakaooacha ombwe jingine la uongozi kwenye taifa hilo la Mashariki ya Kati linalokabiliwa na mzozo wa kisiasa na uchumi unaochechemea.

https://p.dw.com/p/4Uaq3
Libanon Beirut | Riad Salameh, Zentralbankpräsident
Picha: MOHAMED AZAKIR/REUTERS

Salameh, aliyeongoza Benki Kuu ya Lebanon kwa miaka 30, ni miongoni mwa viongozi wanaolaumiwa kwa mzozo wa kiuchumi unaoikumba nchi hiyo ambao umeshuhudia kuporomoka kwa thamani ya sarafu na kupanda kwa kiwango cha umasikini. 

Salameh anawachia wadhifa huo katika wakati mataifa kadhaa ya Ulaya yakitoa waranti wa kumsaka kuhusiana na madai ya uhalifu wa kifedha.

Soma zaidi: Uchumi wa Lebanon waathirika kutokana na mgogoro wa kisiasa

Tabaka tawala nchini Lebanon lilikuwa limeshindwa kuafikiana juu ya mrithi wa Salameh na nafasi yake ingelijazwa kwa muda na mmoja wa manaibu wake wawili. 

Kujiuzulu kwake kunatokea wakati Lebanon inaongozwa na serikali ya mpito na wanasiasa wa nchi hiyo pia wameshindwa kuteua rais mpya kutokana na tofauti zilizopo.