1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaItaly

G7 kukubaliana kuhusu mpango wa dola bilioni 50 kwa Ukraine

13 Juni 2024

Viongozi wa kundi la nchi saba tajiri ulimwenguni la G7 wanaokutana kwa siku ya kwanza ya mkutano wa kilele nchini Italia, wamefikia makubaliano ya kuipa Ukraine dola bilioni 50 wakitumia mali za Urusi zinazozuiliwa.

https://p.dw.com/p/4gz4y
Viongozi wa G7 wakutana nchini Italia
Viongozi wa G7 wakutana nchini ItaliaPicha: Alex Brandon/AP Photo/picture alliance

Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky ameungana na Rais Joe Biden wa Marekani na viongozi kutoka Italia, Uingereza, Ufaransa, Ujerumani na Japan katika eneo la mapumziko la Borgo Egnazia mjini Puglia.

Viongozi hao wamekubaliana kuhusu mkopo wa dola bilioni 50 kuisaidia Kyiv katika ulinzi, bajeti na kusaidia kwa ujenzi mpya baada ya zaidi ya miaka miwili ya vita na Urusi.

Awali, Mshauri wa usalama wa taifa nchini Marekani Jake Sullivan alisema walitarajia kufikia makubaliano kuhusu mpango huo.

Umoja wa Ulaya ulikubaliana mapema mwaka huu kuipa Ukraine faida zitokanazo na mali za Urusi zinazoshikiliwa, kiasi cha hadi euro bilioni tatu kwa mwaka.

Lakini wazo la G7 ni kutumia fedha hizo ili kutoa msaada wa zaidi na wa haraka kupitia mkopo mkubwa wa awali.