1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

FIFA yatangaza sheria mpya 95 za soka

1 Juni 2016

Shirikisho la kabumbu la kimataifa FIFA limezifanyia marekebisho kanuni kadhaa za mchezo unaopendwa ulimwenguni wa dimba. Lengo ni kujaribu kuurahisisha mchezo huo.

https://p.dw.com/p/1Iy8L
Schweiz Zürich FIFA Außerordentlicher Kongress Wolfgang Niersbach
Picha: Reuters/A. Wiegmann

Siku kumi kabla ya kipenga cha kwanza cha michuano ya fainali za kombe la Ulaya nchini Ufaransa, shirikisho la kabumbu la kimataifa FIFA limetangaza marekebisho ya kanuni 95 za dimba yanayoanza kufanya kazi kuanzia leo.

Wanachama wanane wa bodi ya kimataifa ya kabumbu IFAB wameyafuta maneno 10.000 kutoka mwongozo uliokuwa ukitumika hadi sasa. Mengi yanahusiana na mambo madogo madogo ingawa katika baadhi ya vifungu kuna mapinduzi yaliyotokea kuhusiana na kanuni za mchezo.

Miongoni mwa marekebisho yaliyoamuliwa na bodi ya kimataifa ya kabumbu-IFA taasisi inayosimamia kanuni za mchezo ni pamoja na mkwaju wa penati: Yeyote yule, atakaetaka kufanya njama ili kipa akimbilie upande mwengine kabla ya wakati, mfano wa zile mbinu anazopenda kuzitumia mchezaji nyota wa Barcelona, Lionel Messi, basi ataonywa kwa kadi ya manjano. Na wakati huo huo mpira watapewa wachezaji wa timu hasimu. Mbinu za kuvuta wakati hazaitoadhibiwa.

Miongoni mwa sheria zilizorekebishwa ni pamoja na inayohudu upigaji penati.
Miongoni mwa sheria zilizorekebishwa ni pamoja na inayohudu upigaji penati.Picha: picture-alliance/Offside /M. Atkins

Unapoadhibiwa mara tatu

Zaidi ya hayo kuna kifungu cha sheria kinachohusiana na nini kitokea mtu akiadhibiwa mara tatu; katika hali kama hiyo; hadi wakati huu ilikuwa mtu akimchezea ngware mwenzake, au kuugusa mpira kwa mkono ukiwa katika eneo la adhabu, aliyefanya madhambi hayo hupigwa kadi nyekundu, huamuliwa penati au mtu aliyefanya makosa hayo kufungiwa kucheza.

Kuanzia sasa marefa watakuwa na madaraka makubwa zaidi; watakuwa wakitoa kadi nyekundu itakapodhihirika tu aliyefanya madhambi amefanya makusudi. Ikiwa mchezaji amefanya dhambi alipokuwa akijaribu kuuania mpira, hapo kadi ya manjano itatosha.

Kanuni ya tatu inahusiana na mchezaji kutolewa nje ya uwanja. Kadi nyekundu itakuwa ikitolewa sio tu wakati wa pambano bali hata kabla ya pambano, ikiwa mchezaji atajitokeza kutofuata maadili ya mchezo. Licha ya kadi nyekundu lakini timu iliyoadhibiwa itaruhusiwa kuteremsha wanasoka 11 uwanjani.

Muda wa matibabu uwanjani

Marekebisho yanahusiana pia na muda wa matibabu uwanjani. Ikiwa madaktari watafanikiwa kumshughulikia barabara mchezaji kwa muda wa sekunde 20, hapo mchezaji huyo hatolazimika kutoka, anaweza kuendelea kucheza. Hadi wakati huu mchezaji alilazimika kutoka uwanjani anapokuwa anatibiwa bila ya kujali matibabu hayo yatadumu muda gani.

Sheria za FIFA zinahusu pia teknolojia ya Kamera kuamua iwapo goli limeingia kweli ama la.
Sheria za FIFA zinahusu pia teknolojia ya Kamera kuamua iwapo goli limeingia kweli ama la.Picha: imago/Revierfoto

Mwongozo wa kurusha mpira, hadi wakati huu mpira ulikuwa ukivurumishwa mbele, lakini mwongozo mpya umefuta hali hiyo. Mpira unaweza kuvurumishwa upande wowote, kushoto, kulia au hata nyuma.

Muda wa kunywa maji kwa wachezaji

Ama kuhusu muda wa mchezaji kunywa maji-ilikwishabainika wakati wa fainali za kombe la dunia nchini Brazil-wanasoka wanapokuwa katika nchi za joto kali,na masharti ya kunywa maji yanabadilika. Hata hivyo muda huo uliotumiwa kuwaruhusu wanasoka kunywa maji unabidi ufidiwe kwa kurefushwa pambano kwa dakika zile zile.

Mpira siku za mbele utaakuwa ukivurumishwa mikono miwili na sio tena kwa mkono mmoja kama ilivyokuwa ikivumiliwa hadi sasa.

Na mwongozo mwingine unahusiana na kulisakata dimba bila ya viatu. Pindi mwanasoka atatokwa na kiatu uwanjani, pambano halitasitishwa. Aliyefikwa na kisa hicho atabidi kuendelea kucheza akiwa amevaa soksi hadi pambano litakapositishwa.

Mwandishi: Sten-Ziemons,Andreas

Tafsiri: Hamidou Oummilkheir

Mhariri: Mohammed Khelef