1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ethiopia yashindwa kuzuwia ufadhili wa UN wa uchunguzi

1 Aprili 2022

Ethiopia imeshindwa jana kuuzuwia Umoja wa Mataifa, kutoa ufadhili kwa kamati ya kimataifa itakayochunguza ukiukaji wa haki za binadamu uliofanywa na pande zote katika vita vya karibuni nchini humo.

https://p.dw.com/p/49LjT
USA | UN Sicherheitsrat in New York zur Lage in Äthiopien
Picha: Manuel Elias/Xinhua/picture alliance

Kamisheni ya kimataifa ya watalaamu wa haki za binadamu kuhusu Ethiopia, ICHRE, iliundwa Desemba iliyopita, na Baraza la Haki za Bindamua la Umoja wa Mataifa, licha ya upinzani mkali kutoka serikali mjni Addis Ababa.

Ikiongozwa na mwedesha mashtaka wa zamani wa mahakama ya ICC Fatou Bensouda, kimisheni hiyo yenye wajumbe watatu ina mamlaka ya mwaka mmoja ambayo inaweza kurefushwa, kuchunguza ukiukaji uliofanywa tangu kuzuka vita Novemba 2020, kati ya vikosi vya serikali ya Ethiopia na waasi wa kundi la Ukombozi wa Watu wa Tigray, TPLF, kaskazini mwa nchi hiyo.

Kwenye mkutano wa kamati ya bajeti ya Baraza la Umoja wa Mataifa, Ethiopia ilijaribu kuzuwia ufadhili wa kamisheni hiyo lakini ilishindwa kupata kura za kutosha.

Kwa mujibu wa chati inayoonyesha mgawanyo wa kura, wanachama 66 walipiga kura dhidi ya Ethiopia, huku ikiungwa mkono na 27 tu na 39 hawakuwepo.