1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaNigeria

ECOWAS yaombwa kutathmini hatua zake za kushughulikia mizozo

24 Februari 2024

Mkuu wa Jumuiya ya Maendeleo Magharibi mwa Afrika, ECOWAS Bola Tinubu ameiomba Jumuiya hiyo kuzingatia mabadiliko ya kimkakati kama inataka kuyashawishi maataifa yanayotawaliwa kijeshi kurejesha demokrasia.

https://p.dw.com/p/4cq44
Mkutano wa ECOWAS, Abuja, Nigeria
Mwenyekiti wa Jumuiya ya Maendeleo magharibi mwa Afrika, ECOWAS, na Rais wa Nigeria Bola Tinubu akizungumza kwenye mkutano usio wa kawaida wa wakuu wa mataifa hayo mjini Abuja, Februari 24, 2024Picha: Kola Sulaimon/AFP/Getty Images

Tinubu amesema jumuiya hiyo inapaswa kuzingatia mabadiliko hayo ili kuweza kuyarejesha mataifa yaliyojitoa kwenye muungano huo.

Amesema hayo katika ufunguzi wa mkutano wa wakuu wa nchi wanachama wa jumuiya hiyo unaofanyika mjini Abuja.

Viongozi hao wanakutana kuzungumzia mzozo wa kisiasa katika ukanda huo uliokumbwa na mapinduzi ya kijeshi na kuchochewa na hatua ya mwezi Januari ya Niger, Burkina Faso na Mali kujitoa kwenye jumuiya hiyo yenye wanachama 15.

Ingawa hakufafanua zaidi, lakini matamshi ya Tinubu huenda yakaongezea nguvu na matarajio ya ECOWAS inayojiandaa kupunguza au kuiondolea vikwazo Niger, ambavyo ni pamoja na kusimamisha uanachama wake kwenye soko la fedha la kikanda na Benki Kuu.