1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Dortmund wapepea, Lewandowski moto

26 Agosti 2019

Borussia Dortmund wameuendeleza mwanzo wao mwema wa msimu baada ya kuwalaza FC Köln nyumbani kwao. Dortmund wanapigiwa upatu kufanya vyema msimu huu baada ya kukiimarisha kikosi chao.

https://p.dw.com/p/3OVEa
1. Bundesliga | 2. Spieltag | 1. FC Köln - Borussia Dortmund
Picha: Getty Images/Bongarts/M. Hangst

Ligi Kuu ya Ujerumani Bundesliga ilishuhudia mechi za mzunguko wa pili kuchezwamwishoni mwa wiki iliyopita ambapo siku ya Ijumaa, vinara wa ligi hiyo Borussia Dortmund walikuwa wamewatembelea FC Köln na baada ya Köln kuingia uongozini wa kwanza, Dortmund walijizoazoa katika kipindi cha pili na kuyapindua matokeo ya mechi hiyo na hatimaye kupata ushindi wa magoli matatu kwa moja.

BVB walifungiwa mabao yao na Jadon Sancho, Achraf Hakimi aliyeingia kama mchezaji wa akiba na Paco Alcacer aliyefunga goli lake la tatu la msimu.

Bayern Munich walishinda ugenini

Baada ya kupata ushindi katika mechi yao ya kwanza Bayer Leverkusen waliendeleza mchezo wao wa kuridhisha kwa kuwacharaza Fortuna Düsseldorf magoli matatu kwa moja Jumamosi.

Bayern Munich walikuwa ugenini wakikwaana na Schalke 04 lakini shinikizo la mashabiki wa ugenini halikuwababaisha kwani waliebuka kidedea tatu bila, mshambuliaji wao Robert Lewandowski akipachika wavuni mabao yote matatu katika mechi ambayo mabingwa hao wa Ujerumani waliwapa nafasi wachezaji wao wapya Ivan Perisic na Philippe Coutinho ingawa waliingia kama wachezaji wa akiba.

Bundesliga | FC Bayern München v Schalke 04
Robert Lewandowski akisherehekea goli lakePicha: Imago Images/M. Volkmann

Hapo Jumapili RB Leipzig walipata ushindi wao wa pili msimu huu kwa kuwaduwaza Eintracht Frankfurt mbili moja.

Na sasa baada ya mechi hizo mbili kwa kila timu magoli chungunzima yamefungwa. Jedwali la wafungaji bora linaongozwa na Mpoland Robert Lewandowski mwenye mabao matano kufikia sasa ukizingatia kuwa katika mechi ya kwanza walipotoka sare ya mabao mawili na Hertha Berlin aliyafunga magoli yote mawili ya Bayern na hapo Jumamosi akawafungia miamba hao mabao matatu pia.

Anayemfuata Lewandowski katika ufungaji ni mshambuliaji wa Dortmund Paco Alcacer mwenye mabao matatu kisha kuna wachezaji wanne wenye mabao mawili Jadon Sancho wa Borussia Dortmund, Luka Waldschmidt wa Freiburg, Timo Werner wa Leipzig na Streli Mamba wa SC Paderborn 07 ndio walio kwenye orodha hiyo.