1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Dar Es Salaam. Viongozi wa mataifa tajiri wahimizwa kuisaidia zaidi Afrika.

15 Julai 2006
https://p.dw.com/p/CG7S

Mkuu wa benki ya Dunia Paul Wolfowitz amerudia wito wake jana kwa nchi tajiri kuongeza misaada kwa Afrika,bara masikini zaidi duniani, kufuta umasikini na kusaidia maendeleo.

Wolfowitz, ambaye yuko nchini Tanzania katika kituo chake cha pili katika ziara yake ya mataifa sita barani Afrika ambayo itakatizwa mwishoni mwa juma hili atakapokwenda nchini Russia kuhudhuria kikao cha viongozi wa mataifa tajiri duniani G8, pia ameyataka mataifa ya Afrika kuimarisha juhudi zao katika maeneo mawili. Amesema kuwa ametiwa moyo na mafanikio makubwa katika maeneo mengi ikiwa ni pamoja na ukuaji wa uchumi, elimu na afya, lakini mataifa hayo yanapaswa kufanya juhudi zaidi kuendeleza ama kuongeza kasi juu ya masuala hayo, amewaambia waandishi wa habari mjini Dar Es Salaam.Amesema kuwa kundi la mataifa ya G8 yamepiga hatua lakini yanapaswa kufanya zaidi katika kutimiza ahadi zao kwa Afrika zilizotolewa katika mkutano wao nchini Scotland mwaka 2005.