1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Covid-19 yatishia sekta ya elimu nchini Uganda

Lubega Emmanuel 1 Juni 2021

Wimbi jipya la maambukizi ya COVID-19 linatishia shughuli za elimu nchini Uganda. Hii ni kufuatia idadi kubwa ya wanafunzi kugunduliwa kuwa na virusi vya ugonjwa huo ambao wataalamu wanaelezea ni aina mpya ya kirusi.

https://p.dw.com/p/3uIJQ
Kansanga Grundschule in Kampala
Picha: DW/M. Hartlep

Wadau wakiwemo wazazi wanaelezea kuwa hii itasababisha masomo kwa wanafunzi wa madarasa ya chini kutoanza wiki ijayo kama ilivyokuwa imepangwa na serikali.

Shule 29 katika wilaya 17 sehemu mbalimbali za Uganda zimefungwa kufuatia kugunduliwa kwa wagonjwa wa COVID-19, wengi wao wakiwa vijana na watoto. Baadhi ya wanafunzi waliogunduliwa kuwa na virusi hivyo, wameagizwa kurudi nyumbani huku wengine wakitengwa maeneo maaluum.Corona: Uganda yaanza zoezi la utoaji chanjo

Madarasa ya juu katika shule za msingi yamekuwa yakiendesha masomo na walimu walitarajia kuwapokea tena wanafunzi wa madarasa ya chini mwishoni mwa wiki hii kuwandaa kuanza tena baada ya kipindi cha miezi kumi na minane. Lakini kufutia wimbi hilo jipya ambalo linaathiri zaidi vijana na watoto, huenda mipango hiyo ikaahirishwa.

Uganda I Impfstoff AstraZeneca
Afisa wa magereza akipatiwa chanjo ya Covid-19Picha: Badru Katumba/AFP/Getty Images

Hali hii ya janga la COVID-19 imekumba hata vyuo vikuu na taasisi za mafunzo ya afya na ufundi. Katika Chuo Kikuu cha Kyambogo, makamu mkuu wa chuo amenukuliwa kutangaza kuwa wanafunzi 50 na wahadhiri wanane wamegunduliwa kuwa na virusi vya corona na ndiyo amependekeza uwanja wa kitaifa wa michezo utengewe wanafunzi kutoka chuo hicho.

Wanafunzi wa kike kwa upande wao wanaelezea kuwa kipindi hiki cha COVID-19 kimelitatiza mfululizo wa mafunzo wamejikuta katika mashaka mengine.

Wiki iliyopita wanafunzi wa chuo hicho walifanya maandamano kupinga agizo la wakuu wa chuo kwamba masomo yote yaendeshwe kupitia mtandaoni. Kulingana na wanafunzi si wote wanaweza kugharimia utaratibu huo na kwa mafunzo mengine utendaji unakuwa shida kufanya hivyo.

Rais Yoweri Museveni anatarajiwa kutangaza hatua mpya za kudhibiti kusambaa kwa COVID-19. Hii itakuwa baada ya kufanya mashauriano na kikosi kazi maalum kinachoshughulikia ugonjwa huo. Kile ambacho baadhi ya raia wanahofia ni kwamba huenda hatua kali ikiwemo kusimaishwa kwa shughuli za masomo na huduma mbalimbali zitatolewa.