1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaAfrika Kusini

Chama cha ANC chafungua kampeni za uchaguzi

24 Februari 2024

Chama tawala nchini Afrika Kusini cha African National Congress, ANC kimefungua pazia la kampeni za uchaguzi hii leo, kikiwa na matumaini ya kuwabakisha wafuasi wake waliokata tamaa.

https://p.dw.com/p/4cq47
Rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa
Rais Cyril Ramaphosa wa Afrika Kusini akiondoka na wajumbe wengine wa Kamati kuu ya chama cha ANC kwenye mkutano uliofanyika mjini Johannesburg, Disemba 5, 2022. Chama hicho kimezindua kampeni zake za uchaguzi huku kikikabiliwa na shinikizo. Picha: Jerome Delay/AP Photo/picture alliance

Chama cha ANC kinaangazia namna ya kukabiliana na ghadhabu iliyochochewa na ukosefu wa ajira, kuzorota kwa uchumi na kuutetea wingi wa wafuasi wake waliodumu kwa miongo mitatu iliyopita.

Akitangaza uzinduzi wa ilani ya uchaguzi mkuu wa Mei 29, kiongozi wa chama hicho rais Cyril Ramaphosa ameahidi kukitumia kipindi cha miezi mitatu iliyosalia kuwaeleza wafuasi wao juu ya umuhimu wa ANCkusalia kama chaguo bora katika uchaguzi wa 2024.

Aidha ameahidi kufanya mchujo wa kina kwa wagombea wa nyadhifa mbalimbali kupitia chama hicho ambao wameonekana kukumbwa na kashfa katika siku za karibuni.

Chini ya uongozi wa Rais Cyril Ramaphosa ANC imeshuhudia kupungua kwa kiasi kikubwa uungwaji mkono kutokana na madai ya ufisadi na matumizi mabaya ya ofisi na sasa kinakabiliwa na kizingiti kikubwa cha kutetea wingi wa kutosha bungeni katikati ya mashaka ya kupoteza katika jimbo muhimu la Kwazulu-Natal.