1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Chakwera aapishwa rais mpya nchini Malawi

28 Juni 2020

Kiongozi wa upinzani aliyetangazwa mshindi katika uchaguzi wa marudio nchini Malawi Lazarus Chakwera ameapishwa kuingia madarakani

https://p.dw.com/p/3eS0j
Malawi Opposition Lazarus Chakwera
Picha: Reuters/E, Chagara

Kiongozi wa upinzani nchini Malawi Lazarus Chakwera ameapishwa kuingia madarakani leo Jumapili na kuwa rais mpya wa nchi hiyo,baada ya kushinda katika marudio ya uchaguzi mkuu.

Chakwera alipata ushindi wa asilimia 58.57 ya kura zote. Sherehe ya kumuapisha rais huyo mpya imefanyika katika mji mkuu wa Malawi Lilongwe.  Katika hotuba yake aliyotoa baada ya kuapishwa amewashukuru Wamalawi akisema wamempa heshima kubwa iliyompa furaha isiyokuwa na kifani.

Rais Chakwera ameongeza kuwaambia wananchi wa Malawi kwamba heshima walioonesha imetokana na nia na kiu chao cha kutaka mabadiliko.

Wamalawi wameamua

Kiasi ya  wapiga  kura  milioni 6.8  katika  taifa  hilo  dogo  la  kusini mwa  Afrika walijitokeza  katika  vituo vya  kupigia  kura  siku  ya Junanne. Na  jana  Jumamosi , tume  ya  mwenyekiti  wa  tume  ya uchaguzi  Chifundo Kachale aliwaambia  waandishi  habari; "Tume imemtangaza Lazarus Chakwera , kwa  kupata  asilimia 58.57 ya kura, kuwa  amechaguliwa  kuwa  rais wa  Malawi.

Malawi | Neuwahlen | Präsidentschaftskandidaten
Picha: Getty Images/AFP/A. Gumulira

Mutharika  alikuwa  wa  pili  kwa  kupata  kura  1,751,377, wakati mgombea  ambaye  hajulikani  sana  Peter Dominico Kuwani amepata  kuwa 32,456.

Watu waliojitokeza  kupiga  kura  ni  asilimia 64.81.

Shangwe ushindi wa Chakwera

Tangazo  hilo lilipokelewa  kwa  shangwe  kubwa  na  vigelegele wakati  waungaji  mkono  upinzani  wakipepea  bendera  ya  Malawi yenye rangi  nyekundu , nyeusi  na  kijani na  kuimba "serikali" katika lugha  ya  Kichechewa.

Mwezi  Februari , mahakama  ya  juu  ya  Malawi  iliona  kuwa uchaguzi  wa  kwanza  umegubikwa  na  mapungufu  mengi , ikiwa  ni pamoja  na  matumizi ya  wino wa  kufanyia  marekebisho kubadilisha  matokeo  katika  karatasi  ya  matokeo.

Malawi Lilongwe | Neuwahlen | Lazarus Chakwera
Picha: Getty Images/AFP/A. Gumulira

Hukumu  hiyo ya kihistoria  imeifanya  Malawi  kuwa  nchi  ya  pili  ya Afrika  kusini  mwa  jangwa  la  Sahara  kubatilisha  matokeo  ya  rais , baada  ya  Kenya  mwaka  2017.

Rais  Mutharika anayeondoka  madarakani wa chama  cha Democratic Progressive Party DPP siku  ya  Ijumaa  alitoa  wito kwa  tume  ya  uchaguzi  ya  Malawi  kubatilisha  matokeo  ya  kura ya  pili na  itangaze uchaguzi  wa  tatu.

Mwandishi: Saumu Mwasimba

Mhariri:Tatu Karema

 

DW Kiswahili | Saumu Mwasimba
Saumu Mwasimba Mhariri na mtangazaji wa Idhaa ya Kiswahili ya DW