1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Serikali ya mpito inatarajiwa kuundwa Pakistan

9 Agosti 2023

Bunge la Pakistan linatarajiwa kuvunjwa na kuundwa kwa serikali ya mpito ya watalaamu itakayosimamia uchaguzi ambao hautamjumuisha mwanasiasa maarufu nchini humo, Waziri Mkuu wa zamani, Imran Khan.

https://p.dw.com/p/4Uwkk
Pakistan Politik I Imran Khan
Picha: Anjum Naveed/AP/picture alliance

Kwa mujibu wa sheria, uchaguzi unapaswa kufanyika ndani ya siku 90 baada ya kuvunjwa kwa Bunge, lakini serikali inayomaliza muda wake tayari imeonya kuhusu uwezekano wa kucheleweshwa kwa uchaguzi huo.

Nchi hiyo inayokabiliwa na matatizo ya kiuchumi, imekuwa katika msukosuko wa kisiasa tangu Khan alipoondolewa madarakani mwezi Aprili mwaka jana.

Mawakili wa Imran Khan kukutana naye baada ya hukumu ya jela

Mwezi huu alihukumiwa miaka mitatu jela kwa makosa ya ufisadi baada ya chama chake kuandamwa kwa miezi kadhaa.

Katika kipindi cha miezi 18 ya uongozi wa Pakistan, vyama vya siasa ambavyo kwa kawaida huzozana na ambavyo viliungana ili kumuondoa Khan madarakani, vimekuwa vikipata uungwaji mkono hafifu kutoka kwa raia wa taifa hilo linaloshikilia nafasi ya tano kwa watu wengi zaidi duniani.