1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bobi Wine kusalia kizuizini bila kikomo

18 Januari 2021

Wasemaji wa jeshi na polisi nchini Uganda wamesema mpinzani wa rais Yoweri Museveni Robert Kyagulanyi Bobi Wine  ataendelea katika kizuizi cha nyumbani kwa muda usiojuliakana.

https://p.dw.com/p/3o5Xi

Vyombo hivyo vya usalama vimedai kuwa na taarifa kuwa akiwa huru, Bobi Wine anapanga kuwachochea vijana kishiriki katika ghasia.


Tangu kutangazwa kwa matokeo ya uchaguzi, Bobi Wine na viongozi wa chama chake cha NUP wamepinga hatua ya tume ya uchaguzi kumtangaza rais Yoweri Museveni kuwa mshindi.

Kulingana na wasemaji wa majeshi na polisi wamepata taarifa za kuaminika kuwa makundi ya vijana walikuwa wameandaliwa kufanya vurugu kwenye barabara kuu za kuingia na kutoka mji wa Kampala na ndiyo sababu kubwa ya kuhakikisha kuwa uvunjaji sheria wa aina hiyo hautokei.

Afrika Uganda Wahlen Bobi Wine, Popstar und Präsidentschaftskandidat der Opposition
Bobi Wine alionekana kwa mara ya mwisho hadharani wakati akipiga kura kwenye uchaguzi Alhamisi iliyopita.Picha: Jerome Delay/dpa/AP/picture alliance

Chama hicho kinahoji kwa nini matokeo kutoka vituo 1,257 hayakujumuishwi kwenye matokeo hayo huku vituo 271 kati ya hivyo vikiwa katika wilaya ya Wakiso ambayo ni ngome kuu ya Bobi Wine.

Chama cha NUP kinalenga kuupinga ushindi wa Museveni 

Chama hicho sasa kinaandaa ushahidi kuwasilisha rufaa mahakamani kupinga matokeo hayo. Lakini kisa cha majeshi na polisi kuvamia makao makuu ya chama hicho asubuhi ya Jumatatu na kuwazuia watu kuingia wala kutoka kimetajwa kuwa kitakwaza shughuli ya kukusanya ushahidi wanahitaji kuwasilisha mahakamani. 

Tansania Chato 2020 | Yoweri Museveni, Präsident Uganda
Rais Yoweri Museveni wa Uganda alitangazwa mshindi kwa muhula wa sita madarakani.Picha: Tanzania State House/Xinhua News Agency/picture alliance


Wakati huohuo, polisi imethibitisha kuwa watu wanne akiwemo mama mjamzito wamepoteza maisha yao kufuatia ghasia zilizozuka mjini Masaka kusini mwa nchi baada matokeo ya urais kutangazwa.

Wagombea wengine wa urais nao wamepinga matokeo hayo hasa kwa kudai kuwa idadi ya wapiga kura ilikuwa kubwa kuliko ile ya watu milioni 10 hivi waliotajwa kushiriki.

Kulingana na tume ya uchaguzi waliosajiliwa kupiga kura ni watu zaidi ya milioni 18.