1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaMarekani

Biden azungumza juu ya uungwaji mkono kwa Ukraine

4 Oktoba 2023

Rais Joe Biden amefanya mazungumzo na washirika muhimu wa Marekani kwa dhamira ya kuwahakikishia uungaji mkono wa Washington wa kuendelea kuisaidia Ukraine katika vita vyake dhidi ya Urusi.

https://p.dw.com/p/4X6Uc
Rais Joe Biden akizungumza na baraza lake la mawaziri
Rais Joe Biden akizungumza na baraza lake la mawaziriPicha: Susan Walsh/AP Photo/picture alliance

Rais Biden amezungumza usiku wa kuamkia leo kwa njia ya simu na viongozi wakuu wa Uingereza, Canada, Ujerumani, Italia, Japan, Poland, Romania na waziri wa mambo ya kigeni wa Ufaransa.

Vilevile alifanya mawasiliano na wakuu wa Umoja wa Ulaya na Jumuiya ya Kujihami ya NATO wote akiwapa ahadi kwamba Marekani haitabadili msimamo wake wa kuisaidia Ukraine kujilinda mbele ya hujuma za Urusi.

Mazungumzo hayo yamenuwia kutuliza hamkani iliyotokea kufuatia uamuzi wa Bunge la Marekani wa kuondoa msaada ziada kwa Ukraine uliopendekezwa chini ya bajeti ya muda iliyopitishwa wiki iliyopita.

Utawala wa Biden ulishindwa kuwashawishi wabunge hasa wenye misimamo mikali wa chama cha Republican kuidhinisha msaada wa nyongeza kwa Ukraine wa kiasi dola milioni 300 kwa Ukraine.