1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaMarekani

Biden alaani shambulizi la shule huko Nashville

Daniel Gakuba
29 Machi 2023

Rais wa Marekani Joe Biden amesema anapanga kuutembelea mji wa Nashville kukutana na familia zilizowapoteza wapendwa wao katika shambulizi la bunduki kwenye shule moja mjini humo.

https://p.dw.com/p/4PQS2
USA Nashville Covenant School  Trauer nach Amoklauf
Picha: John Amis/AP

Watu sita waliuawa katika shambulio hilo la Jumatatu wiki hii, wakiwamo wanafunzi watatu na wafanyakazi watatu. Biden alikemea alichokiita 'uhalifu wa kuchukiza wa kutumia bunduki dhidi ya watoto', na kuongeza kuwa kama taifa, Wamarekani wanapaswa kusimamisha kadhia hii. Alisema ''Unajua, tunalazimika kuwajibika zaidi, kuwalinda watoto wetu ili wajifunze kusoma na kuandika badala ya kukwepa risasi madarasani. Tunalazimika kuchukua hatua.''

Akizungumza jimboni North Carolina, Biden alisema mashambulizi ya kutumia silaha za moto yanauwa Wamarekani wengi wenye umri kuanzia mwaka mmoja hadi miaka 19, kuliko wanaokufa katika ajali za barabarani. Rais huyo alisema sehemu kubwa ya Wamarekani wanaamini kuwa umiliki wa silaha za kivita ni kitu kisichoeleweka, na kulitolea wito bunge la Marekani kupiga marufuku ununuzi wa silaha za aina hiyo.