1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

BEIRUT.Koffi Annan ziarani mashariki ya kati

29 Agosti 2006
https://p.dw.com/p/CDH9

Katibu mkuu wa umoja wa mataifa Koffi Annan ambae ameanza ziara katika mashariki ya kati yenye lengo la kusisitiza mkataba uliotiwa saini wa kusimaishwa vita kati ya Israel na wapiganaji wa Hezbollah leo hii anatarajiwa kuzuru Lebanon.

Annan atazuru kusini mwa Lebanon kujionea hali ilivyo katika eneo hilo baada ya vita vya siku 34 vilivyokumba eneo hilo.

Bwana Annan alianza ziara yake ya mashariki ya kati hapo jana aliihimiza Israel kuondosha vizuizi vyake kutoka ili kutoa fursa ya kufikishwa misaada ya kiutu kwa wahanga wa vita nchini Lebanon wakati huo huo bwana Annan pia amewataka wanamgambo wa Hezbollah kuwaa achilia wanajeshi wawili wa Israel waliowateka nyara.

Katibu mkuu amesema kwamba nchi za ulaya zimejitolea kuwapeleka wanajeshi wake 9000 katika kikosi cha kimataifa cha kulinda amani nchini Lebanon.

Annan pia amesema kwamba atapendekeza kwa Syria izuie uingizaji wa silaha kinyume cha sheria kuelekezwa kwa wanamgambo wa Hezbollah.

Wakati huo huo waziri mkuu wa Israel Ehud Olmert ameanzisha uchunguzi juu ya vita vya Lebanon.