1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Baerbock ziarani Mashariki ya Kati mwishoni mwa juma

Sylvia Mwehozi
5 Januari 2024

Waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani Annalena Baerbock mwishoni mwa juma atatembelea Israel katika ziara yake ya nne tangu kuzuka kwa vita vya Gaza.

https://p.dw.com/p/4auTO
 Annalena Baerbock
Waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani Annalena BaerbockPicha: Michael Kappeler/dpa/picture alliance

Msemaji wa wizara ya mambo ya nje ya Ujerumani Sebastian Fischer aliuambia mkutano wa kawaida na waandishi wa habari siku ya Ijumaa kwamba Baerbock atafanya mazungumzo na waziri mpya wa mambo ya nje wa Israel, Israel Katz, pamoja na Rais Isaac Herzog.

Pia atakutana na rais wa mamlaka ya Palestina Mahmud Abbas na waziri wa mambo ya nje Riyad al-Maliki.

 Baerbock mjini Cairo
Waziri wa Mambo ya Nje wa Misri Sameh Shoukry (kulia) akutana na mwenzake wa Ujerumani Annalena Baerbock mjini Cairo Oktoba 2023Picha: Ahmed Hasan/AFP

Baerbock baadaye atasafiri kwenda Misri kukutana na waziri mwenzake Sameh Shoukry na pia alipanga kuzuru Lebanon.

Soma hapa: Ujerumani yahimiza uwajibikaji wa kimataifa katika ukanda wa Gaza

Mazungumzo hayo yatazingatia "hali ya kushutusha ya kibinadamu huko Gaza, hali ya Ukingo wa Magharibi na hali tete katika mpaka wa Israel na Lebanon", pamoja na juhudi za kuachiliwa kwa mateka zaidi wa Hamas.

Katika mkutano na waandishi wa habari siku ya Ijumaa, Baerbock alisema kwamba Waisraeli na Wapalestina "wataweza tu kuishi bega kwa bega kwa amani ikiwa usalama wa mmoja unamaanisha usalama wa mwingine".

Annalena Baerbock na Mohammad Shtayyeh
Waziri Mkuu wa Palestina Mohammad Shtayyeh akipeana mkono na Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani Annalena Baerbock mjini RamallahPicha: Ammar Awad/REUTERS

Hofu imezidi kutanda kuwa huenda mzozo kati ya Israel na Hamas ukaenea baada ya mmoja wa viongozi wa kundi hilo la wanamgambo kuuawa katika viunga vya Beirut.

Soma kuhusu taarifa hii: Baerbock: Ujerumani inatumai Israel itazuia madhila kwa Wapalestina

Mbali ya mauaji hayo ambayo yanadhaniwa kuwa yamefanywa na Israel, jeshi la Israel limekuwa kwa miezi kadhaa katika makabiliano ya risasi kwenye mpaka na wanamgambo wa Hezbollah.

Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Antony Blinken pia alianza ziara yake siku ya Alhamisi huko Mashariki ya Kati, ikiwa ni pamoja na Israel, naye pia kiwa ni ziara yake ya nne tangu vita kuanza.