1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaIran

1,000 washitakiwa kwa kuandamana Iran

8 Novemba 2022

Mahakama nchini Iran imearifu leo kwamba, zaidi ya mashitaka 1,000 yanayohusiana na maandamano ya hivi karibuni nchini humo yamewasilishwa mahakamani kutokea jimbo la Tehran pekee.

https://p.dw.com/p/4JBwK
Iran I Szenen aus den Protesten im Iran und Slogans der Demonstranten
Picha: UGC

Msemaji wa mahakama nchini Iran Masoud Setayeshi amearifu hayo mapema hii leo, akisema zaidi ya watu 1,000 wamefunguliwa mashitaka yanayohusiana na maandamano hayo.

Tangu kifo cha binti huyo Mahsa Amini akiwa mikononi mwa polisi ya maadili Septemba 16, kwa madai ya kukiuka kanuni za mavazi ya wanawake, Iran imekumbwa na maandamano ya nchi nzima na ambayo yanachukuliwa kama miongoni mwa kizingiti kikubwa kabisa dhidi ya watawala wa kidini nchini humo tangu mapinduzi ya mwaka 1979.

Setayeshi amesema, kwa sasa umma na hata waandamanaji wasioyaunga mkono maandamano ya kuipinga serikali, wanazitaka taasisi za kiusalama kuwachukulia hatua kali watu wachache waliosababisha mtafaruku.

Soma Zaidi:Kifo cha msichana Mahsa chazusha maandamano makubwa Iran 

Siku ya Jumapili, idadi kubwa ya wabunge wa Iran waliitaka kuchukuliwa hatua kali za kisheria dhidi ya wale waliowataja kama maadui wa Mungu. Azimio hilo liliidhinishwa na wabunge na wabunge 227. Wabunge hao walisema maafisa wa serikali na mahakama wanatakiwa kutumia mfumo wa "jicho kwa jicho" dhidi ya wale watu walioharibu maisha na mali kwa kutumia silaha.

Iran Unruhen l Anti-Hijab-Proteste in Qom l Verunstaltung des Porträts des Führers Ayatollah
Waandamanaji wa Iran wamekuwa wakipambana kuondolewa kwa utawala wa sasa pamoja na sheria kali dhidi ya wanawake. Picha: SalamPix/ABACA/picture-alliance

Soma Zaidi: Raia wa Iran waendelea kuandamana licha ya onyo la Mahakama

Wabunge hao pia waliitaka mahakama kuwashughulikia ipasavyo wahusika wa uhalifu huo na kuwashughulikia wale wote waliochochea ghasia hizo, wakiwemo baadhi ya wanasiasa. Mapema siku ya Jumapili, vyombo vya habari na Kikosi cha Walinzi wa Mapinduzi, walisema maafisa wanne wa polisi na mtu mmoja waliyemtaja kama gaidi waliuawa katika matukio tofauti kufuatia ghasia hizo.

Mapema jana, katibu mkuu wa chama cha upinzani cha Union of Isalmic Iran People, Azar Mansouri, aliandika kupitia ukurasa wake wa twitter akishinikiza kufanyika kwa uchaguzi mpya akisema ndio namna pekee ya kumaliza machafuko ya tangu kifo hicho.

Amesema pamoja na uchaguzi ambao utahallalisha viongozi wa kisiasa, kuna umuhimu pia wa kuimarishwa kwa utawala wa sheria na kuongeza kuwa wale walio madarakani wanalazimika ia kushughulikia chanzo cha maandamano na machafuko hayo badala ya kutoa udhuru kila wakati.

Kulingana na wanaharakati wa haki za binaadamu, zaidi ya watu 300 wamekufa katika machafuko hayo na zaidi ya 14,000 wameziuwa kwenye vizuizi mbalimbali nchini humo. Vyombo vya habari vya nchini humo aidha viliarifu mwezi uliopita kwamba wanajeshi 46 wa vikosi vya usalama ikiwa ni pamoja na maafisa wa polisi waliuawa.

Soma Zaidi: Watu 31 wauawa kwenye maandamano nchini Iran

Katika kile kinachoonekana ni hatua ya Iran kuendelea kuyakosoa mataifa ya magharibi juu ya  maandamano hayo, jana Jumatatu, Iran ilimuita balozi wa Norway, ikipinga kile ilichoita matamshi ya uingiliaji yaliyotolewa na spika wa bunge la Norway aliyeunga mkono maandamano hayo ya kuipinga serikali. Tehran imekuwa ikiyatuhumu mataifa ya kigeni kwa kuchochea maandamano hayo. Hii ilikuwa ni mara ya pili kwa balozi huyo kuitwa na wizara ya mambo ya nje ya Iran katika kipindi cha miezi miwili iliyopita.

Tizama Zaidi: 

Mashirika: RTRE/DPAE