1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUkraine

Zelensky ateta na Orban uanachama wa Ukraine Umoja wa Ulaya

11 Desemba 2023

Rais Volodymyr Zelensky wa Ukraine amezungumza na waziri mkuu wa Hungary, Viktor Orban kuhusu dhamira ya nchi yake ya kutaka kujiunga na Umoja wa Ulaya.

https://p.dw.com/p/4a0UK
Rais Volodymyr Zelensky wa Ukraine
Rais Volodymyr Zelensky wa UkrainePicha: AFP/Getty Images

Katika hotuba yake kwa njia ya video jana jioni rais huyo wa Ukraine amesema amekuwa muwazi kadri awezavyo katika mazungumzo yake na kiongozi huyo wa Hungary kuhusiana na suala hilo.

Msemaji wa Orban, Bertalan Havasi amesema waziri mkuu huyo ameweka wazi kwa Zelensky kwamba wanachama wa Umoja wa Ulaya bado wanaendelea na majadiliano.

Hivi karibuni waziri mkuu huyo wa Hungary alitishia kuyazima matumaini ya Ukraine ya kuanza mapema kwa mazungumzo na Umoja huo kuhusu dhamira yake ya kutaka kuwa mwanachama.

Mazungumzo ya rais Zelensky na waziri mkuu wa Hungary yamekuja wakati kiongozi huyo wa Ukraine akiwa ziarani Buenos Aires alikohudhuria shughuli ya kuapishwa rais mpya wa Argentina Javier Milei.

Zelesky anatarajiwa kesho Jumanne kukutana na rais Joe Biden mjini Washington.