1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Zelenskiy aituhumu Urusi kwa ugaidi baada ya mauaji ya raia

2 Julai 2022

Makombora yamevurumishwa nchini Ukraine na kuuwa raia wengi na kuwajeruhi wengine kadhaa katika maeneo ya watu wengi mwanzoni mwa wikendi, na kumfanya rais Volodymyr Zelenskiy kuituhumu Urusi kufanya ugaidi wa kitaifa.

https://p.dw.com/p/4DYun
Präsident Selenskyj nimmt  am NATO-Gipfel teil
Picha: UKRAINIAN PRESIDENTIAL PRESS SERVICE/REUTERS

Mashambulizi dhidi ya mji wa mapumziko wa kusini yameuwa watu 21 na wengine kadhaa wengine kujeruhiwa, baada ya makombora kupiga majengo ya makazi na kituo cha mapumziko mjini Sergiyvka, kilomita 80 kusini mwa bandari ya Bahari Nyeusi ya Odessa.

Maroketi yalishambulia majengo ya makazi katika mji wa Solviansk, katikati mwa mkoa unaowaniwa wa Donbas, na kuuwa mwanamke aliekuwa kwenye bustani yake na kumjeruhi mume wake, aliliambia jirani shirika la habari la AFP Jumamosi, akielezea kuwa kifusi kilisambaa katika makazi jirani.

Soma pia: NATO: Urusi ni tishio la moja kwa moja kwa washirika

Shuhuda huyo alisema shambulizi hilo la Ijumaa lilidhaniwa kutumia mabomu ya mtawanyiko yanayosambaa kwenye aneo kubwa kabla ya kulipuka, na kupiga majengo na watu waliokuwa nje.

Ukraine-Krieg | Angriff auf Odessa
Jengo la makazi ambalo limepigwa na makombora ya Urusi na kuuwa raia 17 na kuwajeruhi 31 katika wilaya ya Serhiivka mkoa wa Odessa, Julai 1, 2022.Picha: Metin Aktas/AA/picture alliance

Mashambulizi hayo yalijiri baada ya Moscow kuondoka kwenye maeneo ya kisiwa cha kimkakati katika pigo kubwa  kwa uvamizi wa Moscow.

Wahanga wa mashambulizi ya Sergivyka walihusisha mvulana wa miaka 12, alisema Zelenskiy katika hotuba yake ya kila siku kwa taifa, na kuongeza kuwa karibu watu 40 walijeruhiwa na kwamba idadi ya vifo huenda ikaongezeka.

"Nasisitiza: hiki ni kitendo cha ugaidi wa kukusudia wa Urusi - na siyo aina fulani ya kosa shambulio la ajali la kombora," alisema Zelenskiy.

"Makombora matatu yalipiga jengo la makazi la ghorofa tatu, ambamo hakuna mtu aliekuwa anaficha silaha, au zana zozote za kijeshi," aliongeza. "Watu wa kawaida, raia waliishi humo."

Ujerumani ililaani haraka vurugu hizo.     

"Namna ya kikatili ambayo wavamizi wa Urusi wanachukulia vifo vya raia katika hatua zake na tena inazungumzia hasara ya nyongeza ni kukosa utu na ubeuzi," alisema msemaji wa serikali ya Ujerumani Steffen Hebestreit.

Steffen Hebestreit
Msemaji wa serikali ya Ujerumani Steffen Hebestreit amelaani mauaji ya raia Odessa.Picha: Michael Kappeler/dpa/picture alliance

Mashambulizi hayo yanafuataia hasira ya ulimwengu mapema wiki hii wakati shambulizi la Urusi lilipoharibu kituo cha maduka mjini Kremenchuk, katikati mwa Ukraine, na kuuwa raia wasiopungua 18.

Soma piaZelensky asema Urusi ina sifa za "Dola ya Kigaidi"

Rais Vladmir Putin amekanusha kuwa vikosi vyake vinahusika na shambulizi hilo na Moscow haikuzungumzia mara moja mashambulizi ya Odessa.

Safari ya kujiunga na Umoja wa Ulaya

Siku ya Ijumaa, Zelenskiy alisifu ukurasa mpya katika uhusiano wa Ukraine na Umoja wa Ulaya, baada ya Brussels hivi karibuni kuipatia Ukrane hadhi ya mgombea wa uanachama katika juhudi za Kyiv kujiunga na kanda hiyo yenye wanachama 27, licha ya kwamba uanachama huo unaweza kuchukua miaka.

"Safari yetu ya uanachama haipaswi kuchukua miongo. Tunapaswa kufanikiwa kuikamilisha safari hii haraka iwezekano," Zelenskiy aliliambia bunge la Ukraine.

Soma pia:Maoni: Uwanachama wa Umoja wa Ulaya sasa ubadilike 

Rais wa Halmashauri Kuu ya Umoja wa Ulaya Ursula von der Leyen, akilihutubia bunge la Ukraine kwa njia ya vidio, alisema uanachama "uko karibu" lakini aliwahimiza kufanyia kazi mageuzi ya kukabiliana na rushwa.

Norway, ambayo siyo mwanachama wa Umoja wa Ulaya, siku ya Ijumaa ilitangaza kiasi cha dola bilioni moja za msaada kwa ajili ya Kyiv, ikiwemo kwa ajili ya ujenzi mpya na silaha.

Mehrfachraketenwerfer USA HIMARS
Wizara ya ulinzi ya Marekani imetanganza msaada zaidi wa kijeshi kwa Ukraine, ikiwemo mfumo wa kurusha roketi wa kisasa maarufu Himars, ambao Marekani ilianza kuipa Ukraine mwezi Juni.Picha: abaca/picture alliance

Na wizara ya ulinzi ya Marekani Pentagon ilisema ilikuwa inatuma msaada mpya wa silaha wenye thamani ya dola milioni 820, ikiwemo mifumo miwili ya ulinzi wa anga na roketi zinazotumiwa na mfumo wa kisasa wa Himars ambao Marekani ilianza kutoa kwa nchi hiyo mwezi uliyopita.

Soma pia:Urusi, China zaikosoa NATO baada ya onyo lake

UNESCO yairodhesha supu ya Ukraine kama urithi ulio hatarini

Katika uamuzi ambao ulipooza zaidi uhusiano kati ya Kyiv na Moscow, shirika la utamaduni la Umoja wa Mataifa limeingiza mapishi ya supu ya kitamaduni ya Ukraine ya borshch kwenye orodha yake ya urithi wa kitamaduni ulioko hatarini.

Ukraine inaichukulia supu hiyo ya liche, ambayo kawaida hutengenezwa na viazisukari, kama chakula cha kitaifa ingawa inatumiwa pia sana nchini Urusi, mataifa mengine ya zamani ya Kisovieti na Poland.     

UNESCO ilisema uamuzi huo uliidhinishwa baada ya mchakato ulioharkishwa uliosukumwa na uvamizi wa Urusi nchini Ukraine.

Soma pia: EU yabainisha mkakati wa kuachana na nishati ya Urusi

Tutashinda kote katika vita vya borshsch na katika vita hivi," alisema waziri wa utamaduni wa Ukraine Oleksander Tkachenko kwenye mtandao wa Telegram.

Msemaji wa wizara ya mambo ya nje ya Urusi  Maria Zakharova alisema: Hummus na pilaf vinatambuliwa kama vyakula vya kitaifa vya mataifa kadhaa. Kila kitu kinaukrainishwa."

Kuondoka kisiwa cha Nyoka

Siku ya Alhamisi, wanajeshi wa Urusi walitelekeza maeneo yao kwenye Kisiwa cha Nyoka, ambacho kiligeuka ishara ya upinzani wa ukraine katika siku za kwanza za vita, na kilichoko kando ya njia za usafiri wa meli karibu na bandari ya Odessa.     

Wizara ya ulinzi ya Urusi iliielezea hatua hiyo kama "ishara ya nia njema" iliyokusudiwa kuonesha kwamba Moscow haitaingilia kati juhudi za Umoja wa Mataifa kuandaa usafirishaji wa nafaka kutoka Ukraine.

Lakini Ijumaa jioni, Kyiv iliituhumu Moscow kwa kufanya mashambulizi ya kutumia silaha zilizopigwa marufuku, ikisema Warusi walishindwa "kuheshimu hata matamko yao wenyewe."

Ukraine | Schlangeninsel (Zmiinyi Island, Snake Island)
Kisiwa cha Nyoka cha Ukraine kilicho Bahari Nyeusi ambako wanajeshi wa Urusi wameondoka.Picha: 2022 Maxar Technologies via AP/picture alliance

Katika nyakati za amani, Ukraine ni msafirishaji mkuu wa biadhaa za kilimo, lakini uvamizi wa Urusi umeharibu mashamba na kushuhudia bandari za ukraine zikikamatwa, kuchomwa au kuzingirwa -- na kuibua wasiwasi kuhusu uhaba wa chakula, hasa katika mataifa masikini.

Soma pia: Zelenskiy ataka Urusi itimuliwe FAO

Mataifa ya magharibi yanamshutumu Putin kwa kutumia mavuno yaliokwama kama silaha kuongeza shinikizo dhidi ya jumuiya ya kimataifa, na Urusi imetuhumiwa kuiba nafaka za Ukraine.

Ukraine siku ya Ijumaa iliiomba Uturuki kuikamata meli ya mizigo inayopeperusha bendera ya Urusi ambayo Kyiv ilidai iliondoa kutoka bandari inayokaliwa na Kremlin ya Berdyansk.

Viongozi wa Ufaransa, Ujerumani na Italia wawasili Kyiv

Wanafunzi kurudi darasani kwa mara ya kwanza Kyiv

Wakati mapigano makali yaliendelea mashariki mwa Ukraine, maafisa walisema shule katika mji mkuu wa Ukraine zingefungua tena mwanzoni mwa mwaka mpya wa masomo Septemba 1 kwa ajili ya madara ya kwanza ya kuhudhuriwa na wanafunzi tangu masomo yalipohamia mtandaoni baada ya kuanza kwa uvamizi.

Soma pia: Mkuu wa UN awasili Kyiv kwa mazungumzo

Olena Fidayan, mkuu wa kitengo cha elimu na sayansi mjini Kyiv, alisema maeneo yanayozunguka shule yatakaguliwa kwa ajili ya vilipuzi na hifadhi za mabomu shuleni zinawekewa tena mahitaji muhimu.