1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
JamiiNepal

Zaidi ya watu 59 wafariki nchini Nepal kufuatia mafuriko

Saleh Mwanamilongo
28 Septemba 2024

Watu wasiopungua 59 wamekufa kufuatia mafuriko na maporomoko ya ardhi yaliyosababishwa na mvua kubwa nchini Nepal.

https://p.dw.com/p/4lC6L

Maeneo makubwa ya Nepal yamefurika tangu Ijumaa, na kusababisha mamlaka kuonya kuhusu mafuriko katika mito mingi nchini humo. Mito karibu na mji mkuu, Kathmandu ilipasua kingo zake, na kusababisha kufurika kwa nyumba zilizo kandokando.

Zaidi ya maafisa wa usalama elfu tatu walipelekwa kusaidia juhudi za uokoaji kwa kutumia helikopta na boti za injini. Huku vikosi vya uokoaji vikitumia maboya kuwavuta walionusurika na kuwapeleka kwenye maeneo salama.

Safari zote za ndege za ndani kutoka Kathmandu zilifutwa kuanzia Ijumaa jioni, na kuathiri zaidi ya safari 150.