1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaSudan

Watu 65 wauawa, mapigano yakiongezeka Sudan

4 Februari 2025

Mapigano makali kusini na magharibi mwa Sudan yamesababisha vifo vya takribani watu 65 na kuwajeruhi wengine 130. Maafa haya yanafanyika wakati ambapo vita kati ya jeshi na wanamgambo wa RSF vinazidi kupamba moto.

https://p.dw.com/p/4q0SK
Sudan Omdurman |  Mapambano yanayoendelea
Wanajeshi wa jeshi la Sudan wakipiga doria katika eneo la Khartoum Kaskazini.Picha: Amaury Falt-Brown/AFP

Kwa mujibu wa vyanzo viwili vya kitabibu, katika jimbo la Kordofan Kusini, takriban watu 40 wameuwawa na wengine 70 wamejeruhiwa kufuatia mashambulizi kwenye mji mkuu wa jimbo la Kadugli.

Mji huo, unaodhibitiwa na jeshi la Sudan, ulilengwa katika shambulio ambalo Gavana Mohamed Ibrahim alililaumu kundi la Sudan People's Liberation Movement-North (SPLM-N), linaloongozwa na Abdel Aziz al-Hilu.

Soma pia: Shambulio dhidi ya soko Sudan lauwa watu 54 na kujeruhi 150

Aidha, gavana huyo amesema kwamba shambulizi hilo lililenga kudhoofisha eneo hilo, akiapa kuondoa "vikosi vya waasi" katika milima inayozunguka Kadugli. Katika muda wote wa vita hivyo, wapiganaji wa SPLM-N wamekabiliana na jeshi la Sudan na hata wanamgambo wa RSF katika maeneo tofauti ya jimbo la Kordofan Kusini. 

Mapigano makali pia yalishuhudiwa katika eneo kubwa la magharibi mwa Darfur, mashambulizi ya anga ya kijeshi yaliulenga mji mkuu wa Darfur Kusini, Nyala, na kuwauwa watu 25 na kuwajeruhi wengine 63.

Daglo awapa motisha wapiganaji wake

Sudan | Mohamed Hamdan Daglo
Mkuu wa wanamgambo wa RSF Mohamed Hamdan Daglo amesema lazima wasonge mbele katika uwanja wa mapambano.Picha: Ashraf Shazly/AFP

Kulingana na shahidi mmoja katika eneo hilo aliyezungumza kwa sharti la kutotajwa jina, shambulio hilo lilipiga Wilaya ya Nyala, eneo lililo chini ya udhibiti wa wanamgambo wa RSF.

Katika taarifa RSF imeshutumu jeshi kwa kutumia mabomu dhidi ya raia katika vitongoji kadhaa huko Nyala.

Soma pia: UN yaonya kuhusu mashambulizi ya kulipiza kisasi Sudan

Kiongozi wa wanamgambo RSF, Mohamed Hamdan Daglo ameapa kufukuza jeshi kutoka mji wa Khartoum.

"Endeleeni kusonga mbele na mema yatawajia, Mungu akipenda. Msizingatie kusonga kwao kwenye mtaa wa al-Inqaz au mtaa wa al-Maouna au kwenye Kamandi Kuu. Hawatofurahia Kamandi Kuu kwa muda mrefu."

"Ninawatolea wito mfikirie ni nini tutakachokidhibiti, sio juu ya kile walichokidhibiti. Hapana. Tutachukua nini? Lazima tusonge mbele, lazima tuangalie mbele."

Wakati jeshi la Sudan likisonga mbele katika mji mkuu, msemaji wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Stephane Dujarric alielezea wasiwasi wake kutokana na ripoti za mauaji ya raia huko Khartoum Kaskazini, yanayodaiwa kufanywa na wapiganaji na wanamgambo wanaoshirikiana na jeshi.

Soma pia: Umoja wa Mataifa washtushwa na kiwango cha mauaji ya raia Sudan

Wanamgambo wa RSF na jeshi la Sudan wamekuwa wakishutumiwa mara kwa mara kwa kuwalenga raia na kuyashambulia kwa makombora maeneo ya makazi.