1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Tahadhari yachukuliwa baada ya shambulio la IS Afghanistan

27 Agosti 2021

Maafisa wa usalama wanaosaidia kuwaondoa Waafghanistan wanaoitoroka nchi kutokana na kitisho cha utawala wa kundi la Taliban, wapo katika tahadhari kubwa ya mashambulizi zaidi baada ya shambulizi la IS lililowaua wengi

https://p.dw.com/p/3zYjm
Afghanistan | Nach dem Anschlag in Kabul
Picha: Wakil Kohsar/AFP/Getty Images

Miripuko miwili inayoaminika kufanywa na kundi la dola la kiislamu IS, iliyofuatiwa na miliyo ya risasi, ilisikika nje ya uwanja wa ndege wa Kabul jana jioni. Vidio zilizochukuliwa na muandishi habari wa Afghanistan, zilionyesha miili ikiwa imetapakaa nje ya uwanja huo. 

Kulingana na afisa wa afya nchini humo pamoja na yule wa Taliban idadi ya raia wa Afghanistan waliouwawa imepanda na kufikia watu zaidi ya 72 wakiwemo wapiganaji 28 wa Taliban. Lakini msemaji wa kundi hilo alikanusha kuuwawa kwa wapiganaji waliokuwa wanashika doria nje ya uwanja wa ndege wa Kabul wakati wa shambulio.

Jeshi la Marekani kwa upande wake, limethibitisha kuwapoteza wanajeshi 13 kwa kile walichokieleza kama shambulio la kimkakati.

soma zaidi: Kumeripotiwa mlipuko nje ya uwanja wa ndege wa Kabul

Kamanda wa vikosi vya Marekani nchini Afghanistan, Frank McKenzie, amesema wapo katika tahadhari ya mashambulizi mengine kutoka kwa IS yakiwemo maroketi na mabomu yaliotegeshwa ndani ya magari. Amesema wanafanya kila wawezalo kuwa tayari kukabiliana na mashambulio mengine iwapo yatatokea huku akisema taarifa za kijasusi zinatolewa kwa ushirikiano wa Taliban.

Akizungumza kutoka ikulu ya White House, Rais wa Marekani Joe Biden ameiamuru wizara ya ulinzi, Pentagon, kupanga namna ya kupambana na ISIS iliyokiri kuhusika na shambulio hilo, akisema kamwe Marekani haitolisamehe kundi hilo

IS yasema imewalenga wakalimani na washirika wa jeshi la Marekani

Konflikt in Syrien | IS-Kämpfer
Baadhi ya wapiganaji wa kundi linalojiita dola la kiislamu ISPicha: Uncredited/Militant Photo/dpa/picture alliance

Kundi linalojiita Dola la Kiislamu, IS, ambao ni adui wa kundi la Taliban pamoja na mataifa ya Magharibi, limesema mshambuliaji wa kujitoa muhanga aliwalenga wakalimani na wale wote waliofanya kazi na jeshi la Marekani. 

Hadi sasa haijawa wazi iwapo mshambuliaji huyo alifanya mashambulizi yote mawili au moja lilikuwa bomu la kutegwa, na iwapo risasi zilizofyatuliwa zilikuwa za IS au kutoka kwa kundi la Taliban kujibu shambulizi hilo.

Merkel asema jumuiya ya kimataifa lazima ikubali kuzungumza na kundi la Taliban

Wakati huo huo, wanajeshi wa kigeni wanaendelea kukamilisha operesheni ya kuwaondoa watu wao na baadhi ya raia wa Afghanistan kabla ya muda wa mwisho waliowekewa na Taliban kwa wanajeshi wote kuondoka nchini humo ifikapo Agosti 31.

Uingereza imesema inatarajia kumaliza operesheni zake ndani ya saa kadhaa zijazo.

Uingereza imefanikiwa kuwaondoa watu 14,000 kutoka Afghanistan wakiwemo Waafghani wenyewe pamoja na raia wa Uingereza tangu Taliban walipoidhibiti nchi katikati ya mwezi Agosti. Ujerumani tayari imemaliza kuwaondoa watu wake na wanajeshi wake hapo jana.

Chanzo: reuters/ap/afp