Wakoptik kumchagua Kiongozi mpya Misri
29 Oktoba 2012Kifo cha Shenuda ambaye aliliongoza kanisa hilo kwa miongo minne, kilianzisha mjadala wa kumchagua kiongozi mpya kuongoza jamii hiyo katika utawala wa baada ya mapinduzi nchini Misri, ambao unakumbwa na ongezeko la hofu ya kimadhehebu. Bruce Amani na mengi zaidi
Wagombea watano, ikiwa ni pamoja na maaskofu wawili na watawa watatu wanaume, wanawania nafasi ya kuwa Baba Mtakatifu wa 118 wa kanisa hilo barani Afrika. Baraza la viongozi wakuu, maafisa wa umma wa saa na wa zamani katika kanisa hilo, wabunge, madiwani na waandishi habari watapiga kura ya kuchagua mgombea wanayemtaka. Majina ya wagombea watatu watakaopigiwa kura nyingi kisha yataandikwa kwenye vijikaratasi tofauti na kuwekwa kwenye sanduku litakalokuwa juu ya madhabahu ya kanisa la mtakatifu Marko mjini Cairo.
Mnamo Novemba nne, mtoto mmoja atafungwa macho yake kwa kitambaa na kuombwa achague moja kati ya karatasi hizo. Mtu atakayechaguliwa ataapishwa katika sherehe itakayoandaliwa tarehe 18 Novemba. Wagombea hao ni pamoja na Askofu Rafael mwenye umri wa miaka 54, aliyehitimu kama daktari na askofu msaidizi wa mkoa wa Katikati ya Cairo, Askofu Tawadros wa mkoa wa Nile Delta, Beheira mwenye umri wa miaka 60. Kasisi Rafael Ava Mina, ambaye ndiye mzee kabisa kuwaliko wagombea wengine na miaka 70, Kasisi Seraphim al-Souriani mwenye umri wa miaka 53 na Kasisi Pachomious al-Suriani, mwenye umri wa miaka 49.
Vuingozi hao wamekuwa wakizuru makanisa mbalimbali kote nchini humo kabla ya uchaguzi huo. Waumini wa kanisa la Koptik kote ulimwenguni waliombwa kufunga na kuomba kwa siku tatu kabla ya kupiga kura, na kipindi cha pili cha mfungo kitaanza mnamo oktoba 31.
Kiongozi mmoja ambaye hayuko kwenye orodha hiyo ni Askofu Bishoy aliye na msimamo mkali, kwa sababu ya mashambulzii yake ya dhidi ya madhehebu mengine, katika matamshi yake ya nyuma katika vyombo vya habari ambayo yangeweza kuzusha msuguano wa kimadhehebu nchini humo.
Waumini wa madhehebu ya Koptik nchini Misri ambao wanajumuisha takribani asilimia 10 ya jumla ya idadi ya raia milioni 83, kila mara hulalamika kuhusu ubaguzi na kutengwa, hata wakati nchi hiyo ikiwa chini ya uongozi wa zamani usio wa kiislamu wake rais Hosni Mubarak ambaye aliondolewa mwaka jana.
Kuongezeka maukundi ya wanamgambo wa kiislamu wenye itikadi kali, na kuchaguliwa kwa rais wa kwanza Muislamu Mohamed Morsi kumezusha hofu ya kutokea unyanyasaji wa wakristo wa Koptik licha ya ahadi za kila mara za Morsi kuwa atakuwa rais wa Wamisri wote.
Katika tukio la hivi karibuni, wakristo watano wa madhehebu ya Koptik walijeruhiwa jana Jumapili baada ya makabiliano kuzuka katika kanisa la kijiji kimoja kusini mwa mji mkuu Cairo.
Ghasia hizo zilizuka wakati wanakijiji Waislamu walipojaribu kufunga barabara inayoelekea katika kanisa hilo wakati waumini wa Koptik wakiwasili kanisani humo kuhudhuria ibada ya Jumapili. Utulivu ulirejea katika eneo hilo baada ya polisi kuingilia kati.
Mwandishi: Bruce Amani
Mhariri:Yusuf Saumu