1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wafanyakazi 280 wa huduma za kiutu waliuawa 2023 - OCHA

19 Agosti 2024

Dunia inaadhimisha Siku ya Huduma za Kibinaadamu huku Umoja wa Mataifa ukisema wafanyakazi waliouawa kwenye maeneo yenye migogoro duniani mwaka 2023 ilivunja rikodi, lakini mwaka huu huenda ukawa mbaya zaidi.

https://p.dw.com/p/4jcZn
Kaimu mratibu wa huduma za dharura wa Umoja wa Mataifa, Joyce Msuya, akizungumza kwenye Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa.
Kaimu mratibu wa huduma za dharura wa Umoja wa Mataifa, Joyce Msuya, akizungumza kwenye Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa.Picha: Loey Felipe/UN Photo/Xinhua/picture alliance

Ofisi ya Uratibu wa Masuala ya Kibinaadamu ya Umoja wa Mataifa (OCHA) ilisema siku ya Jumatatu (Agosti 18) kwamba wafanyakazi 280 waliuawa kwenye mataifa 33 katika mwaka 2023.

Hili ni ongezeko la asilimia 137 na zaidi ya mara mbili ya vile hali ilivyokuwa mwaka 2022, ambapo waliouawa walikuwa 118. 

Kaimu Mratibu wa Huduma za Dharura wa Umoja wa Mataifa, Joyce Msuya, alisema vifo vingi zaidi vya mwaka jana vilitokea kwenye Ukanda wa Gaza katika miezi mitatu ya mwanzo ya mashambulizi ya Israel kwenye ukanda huo yaliyoanza mwezi Oktoba. 

Madhara ya kusitisha ufadhili kwa UNRWA

"Hali ya kufanya mashambulizi dhidi ya wafanyakazi wa misaada kuwa jambo la kawaida na ukosefu wa uwajibikaji ni mambo yasiyokubalika, yasiyoingia akilini na yenye madhara makubwa kwa operesheni za misaada popote yanapotokea. Wenye madaraka lazima wachukuwe hatua za haraka kukomesha mashambulizi dhidi ya raia na hali ya wahalifu kutokuchukuliwa hatua." Aliongeza kaimu mratibu huyo.

Wengi zaidi wauawa Gaza

OCHA ilisema kuwa 123 katika vifo hivyo vilikuwa vya wafanyakazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuwahudumia Wakimbizi wa Kipalestina (UNRWA) ambavyo vilitokana na mashambulizi ya anga ya jeshi la Israel.

Miongoni mwa athari za mashambulizi ya Israel dhidi ya majengo ya UNRWA katika Ukanda wa Gaza.
Miongoni mwa athari za mashambulizi ya Israel dhidi ya majengo ya UNRWA katika Ukanda wa Gaza.Picha: EYAD BABA/AFP via Getty Images

Ofisi hiyo ya Umoja wa Mataifa inasema kwamba mwaka huu wa 2024 huenda ukawa mbaya zaidi, kwani kufikia tarehe 7 Agosti, tayari wafanyakazi 172 walishauawa.

Soma zaidi: Ujerumani kuanza tena ushirikiano na shirika la Palestina UNRWA

Taarifa iliyotolewa na OCHA ilizugumzia pia jinsi hali inayozidi kuwa mbaya nchini Sudan na Sudan Kusini ilivyochangia ongezeko hilo la idadi ya wafanyakazi wa huduma za kibinaadamu wanaouawa wakiwa kwenye kazi zao.

Wafanyakazi 25 wameuawa nchini Sudan tangu mwezi Aprili 2023 na wengine 34 nchini Sudan Kusini.

Mashirika yawaandikia wanachama UM

Siku ya Jumatatu (Agosti 19), mashirika ya kibinaadamu kote ulimwenguni yaliyaandikia barua mataifa wanachama wa Umoja wa Mataifa kuyataka yachukuwe juhudi zaidi za kuwalinda wafanyakazi wa misaada wakati ulimwengu ukiadhimisha Siku ya Huduma za Kibinaadamu.

Miongoni mwa athari za mashambulizi ya Israel dhidi ya majengo ya UNRWA katika Ukanda wa Gaza.
Miongoni mwa athari za mashambulizi ya Israel dhidi ya majengo ya UNRWA katika Ukanda wa Gaza.Picha: Abed Khaled/REUTERS

"Tutaendelea kubakia na kuhudumia kwenye maeneo yenye migogoro kote duniani, lakini hali inatutaka tuwe na msimamo wa pamoja na kutoa wito wa kulindwa wafanyakazi wetu, wahudumu wa kujitolea na raia tunaowahudumia." Ilisomeka sehemu ya barua hiyo. 

Soma zaidi:Ujerumani yalaani ongezeko la ghasia dhidi ya UNRWA 

Mbali ya Palestina, Sudan na Sudan Kusini, mataifa mengine yaliyomo kwenye orodha ya nchi kumi zenye mauaji mengi zaidi ya wafanyakazi wa misaada ni pamoja na Israel na Syria, ambako wafanyakazi saba waliuawa kwa kila nchi, Ethiopia na Ukraine, ambako wafanyakazi sita waliuawa kwa kila nchi, Somalia iliyokuwa na vifo vitano, na vifo vinne kwa kila moja kati ya Myanmar na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

Vyanzo: AFP, AP, dpa