1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Vyombo vya usalama vya Tanzania vyalaumiwa kwa mauaji

10 Septemba 2024

Mwenyekiti wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere nchini Tanzania Joseph Butiku amekemea vikali wimbi jipya la utekaji watu pamoja na mauaji huku akivitwika lawama vyombo vya ulinzi na usalama.

https://p.dw.com/p/4kSsR
Tanzania | Bendera ya Tanzania
Taifa la Tanzania limekumbwa na visa vya utekaji na mauaji ya watu wa kada mbalimbali na kuibua ukosoaji juu ya kushindwa kwa mamlaka za usalamaPicha: Valerio Rosati/Zoonar/picture alliance

Taasisi ya Mwalimu Nyerere inatoa tamko hili siku moja baada ya aliyekuwa kiongozi wa chama kikuu cha upinzani Chadema Ali Kibao kuzikwa jana Jumatatu mkoani Tanga baada ya kutekwa na kisha kuuawawa jijini Dar es salaam.

Butiku amesema vitendo vya utekaji, unyanyasaji na mauaji siyo hulka ya Tanzania.

Butiku ambaye alikuwa akuzungumza na waandishi wa habari amesisitiza kuwa  taifa la Tanznaia siyo taifa la wahuni wala wauaji bali ni taifa linaloendeshwa kwa kufuata misingi ya katiba na sheria zake.

Amesema ni muhimu Rais Samia akapewa taarifa sahihi na vyombo vya ulinzi na usalama na kuongeza kuwa licha ya kwamba suala la ulinzi na amani ya nchi ni jukumu la kila raia, lakini vyombo vyenye dhamana katika eneo hilo vinapaswa kuwajibika.

Amesema vyombo hivyo vinajua yale yanayoendelea hivyo haviwezi kukwapa lawama na vinapaswa kuwajibika.

Tangu kuzuka upya kwa wimbi la utekaji na unyanyasaji vyombo vya ulinzi na usalama vimekuwa katikati ya kidole cha lawama huku chama kikuu cha upinzani  kimekuwa kikililaumu jeshi la polisi.

Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan
Rais Samia Suluhu Hassan wa Tanzania ameagiza uchunguzi wa visa vya mauaji na utekaji vinavyoendelea nchini TanzaniaPicha: Presidential Press Service Tanzania

Mauaji ya kiongozi huyo wa Chadema yamelaniwa vikali na viongozi wa kisiasa, taasisi za kiraia pamoja na jumuiya ya kimataifa.

Ubalozi wa Marekani umehimiza kuwepo kwa uchunguzi wa kina ikisema vitendo vya namna hiyo havikubaliki katika uwanda wa demokrasia. Ubalozi wa Canada umeikaribisha hatua ya Rais Samia kuhimiza uchunguzi wa haraka juu ya tukio hilo.

Chadema imepanga kukutana wakati wowote kuanzia sasa kufuatia mauji ya kiongozi wake huyo kabla ya kutoa msimamo wake kwa umma. Viongozi wake wengine watatu wanaodaiwa kutekwa katika siku za hivi karibuni hawajulika waliko hadi sasa.

Kumekuwa na hali ya wasiwasi miongoni mwa  jamii kutokana na kuongezeka kwa wimbi la watu kupotea katika mazingira ya kutatanisha. Hivi karibuni chama cha wanasheria cha Tanganyika Law Society kilitoa orodha ya watu 87 iliyodai wametekwa katika maeneo mbalimbali ya nchi.

Soma pia:Kituo cha Sheria Tanzania chazindua ripoti ya haki