1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroUrusi

Uvamizi wa Ukraine nchini Urusi ni halali asema Stolternbeg

Angela Mdungu
31 Agosti 2024

Katibu Mkuu wa Jumuiya ya kujihami ya NATO Jens Stoltenberg amesema, uvamizi wa Ukraine wa Agosti 6 kwenye mkoa wa Kursk nchini Urusi ni halali.

https://p.dw.com/p/4k85B
Wakati wa mahojiano na gazeti la Bild am Sonntag la Ujerumani, Stoltenberg amesema Ukraine ina haki ya kujilinda
Wakati wa mahojiano na gazeti la Bild am Sonntag la Ujerumani, Stoltenberg amesema Ukraine ina haki ya kujilinda Picha: ROBERTO SCHMIDT/AFP via Getty Images

Jens Stoltenberg amefafanua kuwa kulingana na sheria ya kimataifa, haki hiyo haiishii mpakani. Hata hivyo amekiri kuwa Jumuiya hiyo haikuarifiwa kuhusu mipango ya Ukraine na kwamba haikushiriki katika uvamizi huo.

Wakati huo huo, watu watano wameuwawa na wengine 46 wamejeruhiwa baada ya Ukraine kuushambulia mji wa Belgorod Kusini Magharibi mwa Urusi Ijumaa usiku.

Gavana Vyacheslav Gladkov wa Belgorod amesema, watu 37 kati ya waliojeruhiwa wakiwemo watoto saba wako hospitali kwa matibabu.

Nalo jeshi la ulinzi wa anga la Ukraine limesema limedungua droni 24 kati ya 52 za Urusi katika mashambulizi ya usiku kucha katika mikoa nane kote Ukraine.

Kulingana na jeshi la Ukraine droni 25 aina ya Shahed zilianguka zenyewe na nyingine tatu ziliruka kuelekea Belarus na Urusi. Hakuna ripoti kuhusu majeruhi wala uharibifu mkubwa katika tukio hilo.