1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroSudan

Umoja wa Mataifa kuwawekea vikwazo makamanda wa RSF Sudan

28 Agosti 2024

Kamati ya baraza la usalama la UN inazingatia kuwawekea vikwazo majenerali wawili wa kikosi cha wanamgambo wa RSF Sudan kwa kutishia amani, usalama na utulivu wa nchi hiyo kupitia ghasia na ukiukaji wa haki za binadamu.

https://p.dw.com/p/4jzJf
Sudan | RSF
Kikosi cha wanamgambo cha RSF mjini KhartoumPicha: Mohamed Babiker/Photoshot/picture alliance

Marekani imependekeza rasmi kuwawekea marufuku ya kusafiri na kuzuiwa kwa mali zao mkuu wa oparesheni wa RSF Osman Mohamed Hamid na kamanda wa RSF magharibi mwa Darfur AbdelRahman Juma Barkalla.

Iwapo wawili hao watafanikiwa kuwekewa vikwazo, itakuwa ni mara ya kwanza kwa Umoja wa Mataifa kuweka vikwazo kutokana na vita vinavyoendelea nchini Sudan na ambavyo vilizuka katikati ya mwezi Aprili mwaka uliopita kati ya jeshi la Sudan na kikosi cha wanamgambo cha RSF.

Soma pia: Marekani kuanzisha mazungumzo ya amani ya Sudan, licha ya jeshi kutothibitisha 

Kamati ya baraza la usalama la Umoja wa Mataifa yenye wanachama 15 hufanya kazi kwa muundo wa maafikiano. Iwapo hakuna mtu atakayepinga pendekezo hilo la kuwekewa vikwazo makamanda hao wawili wa RSF kufikia Ijumaa mchana, basi moja kwa moja vikwazo hivyo vitatekelezwa.

Wanachama pia wanaweza kuomba muda zaidi wa kuzingatia pendekezo hilo, kuliweka katika hali ya kusubiri au kulipinga kabisa.