1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ujerumani kukipiga na Uhispania ligi ya Mataifa Ulaya

Sekione Kitojo
31 Agosti 2020

Kandanda la kimataifa  linarejea  baada ya kukosekana kwa muda mrefu kutokana  na  janga  la  virusi vya corona.

https://p.dw.com/p/3hp0t
	
DFB Nationalmannschaft Team
Picha: picture-alliance/GES/M. Gilliar

Baada ya  mapumziko ya zaidi ya  miezi tisa , kikosi cha  timu  ya taifa  ya  Ujerumani kikiongozwa na  kocha  Joachim Loew , na vikosi  vingine  vya  kimataifa   barani  Ulaya , vinarejea uwanjani katika  kinyang'anyiro  cha  Ligi  ya  mataifa. Athari za  janga  la virusi  vya  corona  bado linatikisa  na michezo hiyo itachezwa bila ya mashabiki kuwapo uwanjani.

Bundestrainer Joachim Jogi Löw
Kocha wa timu ya taifa ya Ujerumani Joachim LoewPicha: picture-alliance/GES/M. Gilliar

Kiasi ya  siku 286 zimepita baada ya kuipiga  mweleka Ireland ya kaskazini kwa  mabao 6-1, Joachim Loew anakusanya  kikosi  chake  tena  leo. Die Manschaft itafanya matayarisho  yake mjini Stuttgart kwa muda wa siku  chache tu  kwa ajili  ya pambano  la  Alhamis la Ligi ya Mataifa  dhidi  ya  Uhispania kabla ya kwenda Basel  ambako  kikosi  hicho kitakutana na miamba wa  Uswisi siku  ya  Jumapili. Mashujaa  walionyakua  mataji  matatu msimu huu  wa Bayern Munich Manuel Neuer, Joshua  Kimmich, Leon Goeretzka na  Serge Gnabry wamepumzishwa.

Italia  ambayo inaonekana  kuimarika  tena  ni wenyeji wa  Bosnia siku  ya  Ijumaa, na  Uingereza  inafanya  ziara  Iceland siku  ya Jumamosi. Mabingwa wa  dunia  Ufaransa pia  wanasafiri kwenda Sweden.

Fussball DFB Training und Trainingsspiel, Aachen 05.06.2019
Kikosi cha timu ya taifa ya Ujerumani kikifanya mazoweziPicha: picture-alliance/GES/M. Gilliar

Kai Havertz

Kocha wa Bayer Leverkusen Peter Bosz anaitayarisha timu yake kwa ajili ya michezo ya Bundesliga msimu ujao bila kufikiria kuhusu mchezaji wa kati Kai Havertz na mshambuliaji Kevin  Volland , na kwamba  huenda  wakakamilisha  uhamisho  wao hivi  karibuni. Havertz anahusishwa na  kuhamia Chelsea na  Volland yuko njiani kuelekea Monaco nchini Ufaransa. "Natarajia  kuwa  hatarejea," Bosz  alisema leo kuhusu Havertz , ambaye anajiunga na  kikosi  cha JoachimLoew katika  timu  ya  taifa.

Vilabu 39 vya madaraja ya juu mawili  nchini  Ujerumani vinakutana kwa mkutano  kwa njia  ya  vidio siku  ya  Alhamis  kuendeleza majadiliano  kuhusiana  na  kuwarejesha  mashabiki uwanjani. Hakutakuwa na  suluhisho  la  haraka  ambapo viwanja  vitupu vinatarajiwa  kuendelea  kuwa  tupu  hadi  kiasi  mwishoni mwa mwezi Oktoba baada  ya uamuzi  kupitishwa  wiki  iliyopita  na kansela  wa  Ujerumani  Angela  Merkel  pamoja na  mawaziri wakuu wa  majimbo  kuendelea  na  marufuku dhidi  ya  mikusanyiko mikubwa. 

Italien DFB-Pressekonferenz in Eppan
Mchezaji wa timu ya taifa ya Ujerumani Niklas SulePicha: picture-alliance/GES/M. Ibo Güngor

Kundi la kikazi la  kisiasa  linaangalia  nafsi  kadhaa wakati taasisi inayoendesha  ligi  ya  kandanda  nchini  Ujerumani DFL, imetoa wito wa  suluhisho  la uwajibikaji  hatua  kwa  hatua ikitegemea  na  hali  ya  janga  hilo", huenda kuanzia mwezi Novemba.

Timu  ya  wanawake  ya  Wolfsburg  huenda imepoteza mchezo wake  wa  fainali ya Champions League  dhidi  ya  Olympique Lyon jana  Jumapili  lakini  mabingwa  hao  wa  Bundesliga na kombe  la shirikisho  wanapigiwa  upatu  kutawala soka  la  wanawake tena nyumbani  msimu huu. Wanaanza ligi wakipambana  na  Essen  siku ya  Ijumaa  katika mchezo  ambao ni  kama  marudio ya mchezo wa fainali  ya  kombe  la  shirikisho  msimu  uliopita.